Rais Samia kushiriki Mkutano wa 38 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa AU

 

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan anatarajia kufanya ziara ya kikazi Jijini Addis Ababa nchini Ethiopia kuanzia kesho tarehe 15/02/2025 kushiriki Mkutano wa Kawaida wa 38 wa Wakuu wa Nchi na Serikali wa Umoja wa Afrika (AU).

Mkutano huo unatarajia kuchagua Mwenyekiti mpya wa Umoja wa Afrika kwa mwaka 2025 ambaye atachukua nafasi ya Mwenyekiti wa sasa wa nchi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Mauritania.

Taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu Sharifa Nyanga imesema mkutano huo pia utachagua viongozi wapya wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika ikiwemo Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Makamishna sita.

Vilevile, mkutano utajadili taarifa ya ushiriki wa Umoja wa Afrika kwenye mkutano wa nchi tajiri duniani (G20) utekelezaji wa Ajenda 2063 ya Umoja wa Afrika na Taarifa ya kuhusu masuala ya mabadiliko ya tabianchi.

Mbali na masuala hayo, mkutano pia utajadili ajenda ya kuhusu matumizi ya nishati safi ya kupikia iliyopendekezwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Kabla ya kushiriki mkutano wa 38, Rais Dkt. Samia atashiriki mkutano wa Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika unaofanyika tarehe 14 Februari 2025.

Chapisha Maoni

0 Maoni