Kundi lingine la watalii wa kigeni zaidi ya 100 lawasili Kilwa

 

Hifadhi ya urithi wa utamaduni wa dunia ya Magofu ya Kale Kilwa Kisiwani na Songo Mnara inaendelea kupokea makundi makubwa ya watalii kutoka Mataifa mbalimbali duniani ambapo jana  Februari 15, 2025 imeshuhudia meli ya kifahari ya kitalii (Le Bougainville) ikishusha jumla ya watalii 149 Hifadhini humo, ikiwa ni meli ya 6 kutia nanga katika bandari ya mjini wa Kilwa katika kipindi cha kuanzia Januari - Februari, 2025.

Kwa miongo kadhaa kumekuwa na dhana kwamba wageni wengi wa nje hupendelea zaidi utalii wa kuona wanyamapori kuliko aina nyingine ya utalii, lakini hivi karibuni dhana hiyo imeanza kubadilika kwa kasi ambapo Tanzania imeanza kupokea wageni makundi Kwa makundi wakitembelea katika maeneo ya malikale hususani Hifadhi ya urithi wa utamaduni wa dunia ya Magofu ya Kale Kilwa Kisiwani na Songo Mnara iliyo chini ya usimamizi wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania - TAWA.

Watalii waliotembelea hifadhi hiyo leo wametokea Mataifa ya  Marekani, Uingereza, Ubelgiji, Austalia, Ireland, Seychelles, Ujerumani na Ufaransa huku wengine wakitokea Mataifa ya Ujerumani, Israeli, Ureno na Canada.

Ujio wa meli hizi za watalii wa kigeni kutoka Mataifa mbalimbali ni uthibitisho tosha kuwa Hifadhi hiyo inazidi kuwa kivutio cha Kimataifa na kuwa miongoni mwa maeneo muhimu kwa Sekta ya utalii nchini.

Sambamba na hilo, ujio wa meli hizi pia unaendelea kudhihirisha juhudi kubwa za  kutangaza vivutio vya utalii vya nchi yetu zilizofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia filamu ya Tanzania The Royal Tour zinazidi kuzaa matunda lakini pia  ni ishara ya mafanikio ya mikakati ya Serikali katika kukuza Sekta ya utalii.



        Na. Beatus Maganja - TAWA

Chapisha Maoni

0 Maoni