Ulomi aliyedaiwa kutoweka, amekufa kwa ajali- Polisi

 

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limesema kuwa Daisle Simion Ulomi, aliyekuwa ameripotiwa kwamba amepotea, alifariki dunia baada ya kupata ajali mbaya na pikipiki aliyokuwa akiitumia siku ya Desemba 11, 2024.

Taarifa hiyo imetolewa leo Desemba 16, 2024 na Kamanda wa Polisi wa Kanda hiyo SACP Jumanne Muliro ambapo ameeleza kuwa tarehe 11 Desemba, 2024 Jeshi hilo lilipata taarifa ya kupotea kwake na ndugu hawakuwa wanampata kwenye mawasiliano ya simu, baada ya yeye kuondoka ofisini kwake Sinza na kudai anaelekea Temeke kufuatilia makontena yake ya biashara.

SACP Muliro amesema Ulomi aliondoka eneo lake huku akitumia pikipiki namba MC 415 DQC aliyokuwa akiendesha mwenyewe, ufuatiliaji umefanyika kwa kushirikiana na ndugu na kubainika kuwa Ulomi alipelekwa kituo cha afya cha Makuburi Ubungo External mchana wa tarehe 11 Desemba, 2024 baada ya kupata ajali mbaya na pikipiki aliyokuwa akiitumia, wasamaria wema walimsadia kumpeleka kwenye kituo hicho akiwa hajitambui na hakuwa na kitambulisho chochote.

Awali, Katibu wa Hospitali ya Rufaa ya Mwananyamala, Lydia Nzema akizungumza na waandishi wa habari amesema walipokea mwili wa Ulomi Desemba 11, 2024 ukitokea Zahanati ya Makuburi, ikidaiwa kifo chake kimetokana na ajali.

“Hii ikiwa na maaana kama kituo cha afya alichopelekwa kwa matibabu ilikuwa ni zahanati ya Makuburi, sisi tumepokea kutoka zahanati hiyo mwili ambao haujatambuliwa na tulihifadhi chumba cha maiti kama ilivyo kwa miili mingine,” amesema Nzema.

Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mwananyamala Dk Zavery Benela amesema mwili wa Ulomi ulifikishwa hospitalini hapo na kuhifadhiwa kwenye chumba cha maiti Desemba 11, 2024.


Chapisha Maoni

0 Maoni