Wateja wa hadhi CRDB kupata punguzo la matibabu JKCI

 

Wateja wa hadhi, wastaafu na wafanyakazi wanaopitisha mishahara yao katika benki ya CRDB kupata punguzo la asilimia 50 wanapohitaji kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati wa hafla fupi ya kusaini mkataba wa makubaliano kati ya JKCI na Benki ya CRDB kuendeleza ushirikiano uliopo baina yao na kutoa huduma kwa jamii.

Dkt. Kisenge alisema Benki ya CRDB ni moja ya Taasisi za fedha kubwa nchini inayochangia maendeleo ya jamii katika nyanja mbalimbali ikiwemo sekta ya afya hasa kwa watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa JKCI.

Benki ya CRDB ni moja ya wadau wa kwanza ambao walitambua umuhimu wa kuwekeza katika afya hususan matibabu ya magonjwa ya moyo kwa watoto ambao wengi wao wanatoka katika familia ambazo hazina uwezo wa kulipia gharama za matibabu ya moyo,” alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema tangu mwaka 2017 Benki ya CRDB imechangia kiasi cha shilingi milioni 775 ambazo zimetumika kulipia upasuaji wa moyo kwa watoto 193.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB Bruce Mwile alisema makubaliano waliyoingia na JKCI ni mwanzo wa ushirikiano utakaoleta manufaa kwa wengi katika maeneo ya huduma za matibabu ya moyo kwa kuwawezesha wateja wa CRDB kupata huduma za afya kwa gharama nafuu.

“Ushirikiano wa JKCI na Benki ya CRDB ni mfano mwingine unaoonyesha jinsi tunavyoendelea kujidhatiti kuhakikisha si tu tunawawezesha wateja wetu kutimiza malengo yao ya fedha bali pia mwenendo wao katika kutunza afya zao,” Mwile.

Mwile alisema lengo la ushirikiano huo ni pamoja na kuisaidia jamii ya watanzania kupata huduma bora za afya na kwa urahisi itakayowasaidia kuweza kujenga uchumi imara wa nchi.

“Afya ni nguzo muhimu ya kimaendeleo na kijamii kwani bila afya bora tunakosa nguvu na uwezo wa kufikia malengo yetu ya kiuchumi na kijamii,” alisema Mwile.

Aidha. Mwile alisema JKCI imekuwa mnufaika wa muda wote kupitia mbio za CRDB kwani kinachopatikana katika mbio hizo kiasi kikubwa hupelekwa JKCI kwaajili ya kuwatibu watoto 100 kila mwaka.



Chapisha Maoni

0 Maoni