JTC yatembelea Mto Malagarasi mpaka wa Tanzania na Burundi

 

Kamati ya Pamoja ya Wataalamu ya Uimarishaji Mpaka wa Tanzania na Burundi (JTC) imetembelea Mto Malagarasi ambao ni sehemu ya mpaka wa kimataifa kati ya nchi hizo mbili ili kujionea hali halisi ya eneo hilo.

Uamuzi wa kutembelea eneo hilo la mto Malagarasi ni sehemu ya programu ya kikao cha JTC kinachoendelea katika halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji mkoani Kigoma.

Kikao hicho pamoja na mambo mengine kimepanga kutembelea katika vijiji vya Bukililo na Nyakayenzi upande wa Tanzania na kijiji cha Kamusha nchini Burundi.

Timu hiyo ya wataalamu ambayo kwa upande wa Tanzania iliongozwa na Mkurugenzi Msaidizi idara ya Upimaji na Ramani Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Bw. Samwel Katambi huku upande wa Burundi ikioongozwa na Meja Jenerali Mbonimpa Maurice.

Lengo la kutembelea mpaka huo wa kimataifa ni kuwezesha JTC Kuandaa bajeti na mpango kazi wa uimarishaji mpaka wa kimataifa baina ya nchi hizo mbili.

Kikao cha Pamoja cha Wataalamu (JTC) kimeanza siku ya jumatatu tarehe 18 Novemba 2024 na kimemalizika Ijumaa tarehe 22 Novemba 2024.

Zoezi la uimarishaji mipaka ya kimataifa ni utekelezaji wa makubaliano ya umoja wa Afrika kuwa ifikapo mwaka 2027 mipaka baina ya nchi za afrika iwe imeimarishwa.

Kiongozi wa wa timu ya Tanzania Bw. Samwel Katambi (wa pili kushoto) akifafanua jambo wakati wa Kamati ya Pamoja ya Wataalamu wa Uimarishaji mpaka wa Tanzania na Burundi (JTC) ilipotembelea eneo la Mto Malagarasi uliopo wilayani Kasulu mkoa wa Kigoma. kushoto ni kiongozi wa timu ya wataalamu kutoka Burundi Mhe. Meja Jenerali Mbonimpa Maurice.


Chapisha Maoni

0 Maoni