Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu,
Mhe. Ali Suleiman Ameir Mrembo amesema Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza
la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi, atazindua miradi ya maendeleo na
kuzungumza na wananchi katika mikutano na makongamano mbalimbali.
Waziri Mrembo ameyasema hayo leo,
tarehe 18 Oktoba 2024, katika viwanja vya Ikulu Zanzibar, alipozindua rasmi
kampeni ya Miaka Minne ya Rais Dk. Mwinyi pamoja na nembo maalum.
Aidha, Waziri Mrembo ameeleza kuwa
kampeni hiyo itaanza rasmi kuanzia tarehe 21 Oktoba 2024 hadi tarehe 16 Novemba
2024.
Halikadhalika, Waziri Mrembo amesema
kampeni hiyo itawafikia wananchi kupitia teknolojia ya habari, ikiwemo
televisheni, mitandao ya kijamii, magazeti, na redio za kijamii.
Naye Mkurugenzi wa Shirika la
Utangazaji Zanzibar (ZBC), Ramadhan Bukini, amesema kampeni hiyo itajumuisha
Mawaziri na Watendaji mbalimbali wa Serikali, ambao watazungumzia mafanikio ya
utekelezaji wa miradi ya maendeleo katika kila sekta, kupitia mahojiano
yatakayofanyika katika Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC).
0 Maoni