Udhibiti wa matukio ya moto misituni wazidi kuimarishwa wilayani Mufindi

 

Katika muendelezo wa juhudi za kukabiliana na majanga ya moto wa msituni leo tarehe 18 Oktoba 2024 Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania kupita Shamba la Miti Saohill kwa kushirikiana na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mufindi wamefanya kikao na madiwani, watendaji wa kata pamoja na maafisa tarafa wa  wilaya ya Mufindi ili kujadili juu ya namna kuendelea kukabiliana na matukio ya moto misituni.

Akuzungumza wakati wa Kikao hicho, Katibu Tawala wa Wilaya ya Mufindi Ndg. Mashaka Mfaume amesema kuwa uchumi wa Wilaya ya Mufindi unategemea uwepo wa misitu na biashara ya mazao ya misitu hususani kutoka katika Shamba la Miti Saohill hivyo ni muhimu kuhakikisha kuwa kunakuwa na mikakati ya pamoja ya pande zote kuhakikisha rasilimali za misitu zinatunzwa.

Katika kikao hicho pia aliwakumbusha viongozi wa vijiji wote (Madiwani, Watendaji na Maafisa Tarafa) majukumu yao katika kuhakikisha misitu haithiriwi na moto ikiwa ni pamoja na kusimamia utekelezaji wa sheria na taratibu ndogo ndogo za halmashauri pamoja na zile za vijiji zinahusu matumizi sahihi ya moto zinatekelezwa kwa usahihi na wananchi katika vijiji vyao.

Sambamba na hayo ameelekeza mambo mbalimbali ambayo kiongozi katika eneo husika anaweza kuyafanya ili kudhibiti majanga ya moto ikiwa ni pamoja na utoaji wa elimu na uhamasishaji juu ya madhara ya moto, kushirikiana na wataalam wa misitu, kujenga vikundi vya kujitolea, kufuatilia utekelezaji wa sheria na taratibu za matumizi ya sahihi ya moto pamoja na kuunda timu au kamati za viongozi wa kudhibiti matukio ya moto.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Ndg. Festo Elia Mgina amesema kuwa viongozi katika ngazi za kata na vijiji kuwajibika na kuwa mfano wa kwanza katika utekelezaji wa sheria na taratibu zilizowekwa kuhusu ulinzi wa misitu dhidi ya matukio ya moto kichaa ambayo yamekuwa yakileta hasara kubwa kwa serikali na wananchi katika Wilaya ya Mufindi.

Aidha amewataka madiwani na watendaji wote kuhakikisha sheria na taratibu zilizowekwa zinaendelea kusomwa na kukumbushwa mara kwa mara kwa wananchi katika mikutano ya vijiji ili kuhakikisha madhara yatokanayo na moto yanadhibitiwa na kuepuka athari zinazojitokeza.



Chapisha Maoni

0 Maoni