Dereva wa ajali iliyoua watu tisa atinga kizimbani

 

Dereva wa basi la Asante Rabi Shedrack Swai (37) aliyesababisha ajali iliyoua watu tisa Oktoba 22.2024 eneo la Ukiligulu, wilaya ya Misungwi, mkoani Mwanza amepandishwa kizimbani jana Oktoba 29,2025 katika Mahakama ya wilaya ya Misungwi na kusomewa shtaka la kuendesha gari kwa uzembe katika barabara ya umma lenye makosa 64 yakiwemo ya kusababisha vifo, majeruhi, uharibifu wa miundombinu na mali.

Akisoma shtaka katika kesi ya Trafiki namba 30855/2024, linalomkabili dereva huyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Wilaya ya Misungwi, Esther Marick, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Ramson Salehe akisaidiana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, Lilian Meli amesema mshtakiwa huyo alitenda makosa hayo kinyume na Kifungu cha 41, 63 (2) (b) na 27 (1) cha Sheria ya Usalama Barabarani namba 168 marejeo ya mwaka 2002.

Salehe aliieleza Mahakama hiyo kuwa mshakiwa anashtakiwa kwa makosa 64 yakiwemo ya kuendesha gari kwa uzembe katika barabara ya umma  na kusababisha vifo vya watu tisa, kujeruhi watu 54 na kusababisha uharibifu wa mali pamoja na miundombinu.

“Mshtakiwa (Shedrack Swai) siku ya Oktoba 22, 2024, ukiwa dereva wa gari lenye namba za usajiri T.458 DYD aina ya Yutong basi uliendesha gari hilo kwa uzembe katika barabara ya umma Mwanza-Shinyanga eneo la Kijiji cha Ukiriguru wilayani Misungwi ambapo ulilipita gari lingine bila kuchukua tahadhari na matokeo yake ukaligonga gari lingine lenye namba za usajiri T. 281 EFG aina ya You tong basi  a kusababisha vifo, majeruhi na uharibifu wa mali,” alisema Mwendesha Mashtaka Salehe.

Baada ya kumsomea makosa hayo, mshtakiwa Shedrack Swai alikiri kutenda makosa hayo yote 64 huku Wakili wa Serikali Mwandamizi Lilian Meli akiiomba mahakama kupanga tarehe nyingine kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo ya awali (PH).

Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Wilaya ya Misungwi, Esther Marick alimweleza mshtakiwa kuwa shtaka linalomkabili linadhaminika na hivyo kumtaka kuwa na wadhamini wawili wenye barua za utambulisho kutoka Serikali ya Mtaa, Kitambulisho cha Taifa (Nida) na bondi ya maneno ya Sh5 milioni kila mmoja.

Hata hivyo mshtakiwa alishindwa kukidhi masharti ya dhamana baada ya mdhamini mmoja kukosa kitambulisho halisi cha Taifa cha NIDA hivyo mshtakiwa kupelekwa rumande katika Gereza la Butimba jijini Mwanza hadi masharti hayo yatakapotimizwa.

Hakimu, Esther aliahirisha shauri hilo hadi Novemba 5, 2024 litakapoitwa kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa hoja za awali.

Mshtakiwa alikamatwa na Jeshi la Polisi muda mfupi baada ya kusababisha ajali na taarifa ya kukamatwa kwake ilitolewa na Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Wilbrod Mutafugwa baada ya kukagua eneo la ajali Oktoba 22, 2024. Hata hivyo pia mstakiwa amefungiwa leseni yake ya udereva na kuondolewa madaraja yake yote.



Chapisha Maoni

0 Maoni