JKCI yawataka Wahariri kuhamasisha jamii uchunguzi wa afya

 

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imewataka waandishi wa habari kutumia vyombo vyao kuihamasisha jamii kufanya uchunguzi wa afya zao kwa upande wa magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya moyo.

Wito huo umetolewa jana Jijini Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu alipokuwa akiongea na wahariri wa vyombo vya habari waliofika kufanya uchunguzi wa magonjwa ya moyo katika Kliniki ya JKCI iliyopo Kawe.

“Bado kuna elimu dogo mno kuhusiana na magonjwa yasiyoambukiza nchini hususan kwa magonjwa ya moyo…na hali hiyo si kwa Tanzania pekee hadi katika mataifa yaliyoendelea elimu bado ni ndogo,” alisema Dkt. Shemu.

Amesema kwamba kutokana na hali hiyo wagonjwa wengi wanafika kupata matibabu wakiwa katika hali ambayo sio nzuri, ambayo ingeweza kuzuilika iwapo wangepima afya ya moyo mapema.

“Unapopata maumivu makali ya kifuani upande wa kushoto usipoteze muda kwenda hospitali zingine, haraka sana kimbilia JKCI ili upate matibabu ya haraka kubaini tatizo, kwani kama ni tatizo la moyo mtu anaweza kupoteza maisha muda mchache,” alisema Dkt. Shemu.

Magonjwa ya moyo huja kwakushtukiza, zaidi ya asilimia 60 ya watu wanaopata mstuko wa moyo hupoteza maisha kutokana na kuchelewa kupata huduma za matibabu kwa wakati, alisema Dkt. Shemu.

Ameeleza kuwa “Wenzetu wa mataifa yaliyoendelea wamejitahidi katika kuhakikisha mgonjwa wa moyo anachukuliwa haraka kwa helkopta na kukimbizwa hospitali ambapo majengo yao hospitali zao juu yanasehemu ya kutulia.”

Amesema matatizo ya moyo yanapochelewa kupatiwa tiba katika hatua za awali, tatizo linaongezeka na kuwa kubwa ambapo pia huchangia kuongeza gharama kubwa za matibabu.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile ameipongeza JKCI kwa kuwa na maono ya kuwafikia watu wa aina mbalimbali kuwafanyia uchunguzi wa afya bure kwani bila hamasa kama hizo wapo watu ambao hasingemudu kupima.

Balile ameeleza kwamba katika zoezi hilo la kupitia upimaji wa afya ya moyo lililoanza jana na kukamilika leo wahariri zaidi ya 50 wamejitokeza kwa ajili ya kuangalia afya zao.

Balile pia, ameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa huduma bora wanazozitoa katika Kliniki ya JKCI Kawe iliyopo jengo la Mkapa Health Plaza, ambayo madhari yake ni mazuri na yenye kumvutia mgonjwa.

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete wakiongozwa na Mkurugenzi Mtendaji Dkt. Peter Kisenge wamekuwa wakitoa huduma za tiba mkoba zijulikanazo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services kwa kufanya upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani.



Chapisha Maoni

0 Maoni