TMDA yaonya matumizi ya ARV’s kunenepesha mifugo

 

Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), imesema kwamba imepata taarifa juu ya uwepo wa baadhi ya wafugaji wanaotumia vibaya dawa za kufubaza makali ya Virusi vya UKIMWI (ARV's) ili kunenepesha mifugo yao.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA Dkt. Adam Fimbo imesema mamlaka hiyo inakemea matumizi hayo kwani yana madhara makubwa kwa afya ya jamii.

Imesema kuwa dawa hizo zinatakiwa zitumike kwa ajili ya kufubaza makali ya virusi vya UKIMWI kwa binadamu baada ya mgonjwa kushauriwa na daktari, na hivyo matumizi yake katika kulisha mifugo kuna hatarisha afya ya jamii.

“TMDA inaelekeza wafugaji wote wanaofanya hivyo kuacha mara moja. Aidha, Kuanzia sasa TMDA imeanza uchunguzi wa kina katika mashamba mbalimbali ya mifugo ili kubaini wanaojihusisha na matumizi holela ya dawa na atakayebainika kufanya hivyo, atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kuharibiwa kwa mifugo yake kwani itakuwa mazao ya mifugo husika haifai tena kwa matumizi ya binadamu,” imesema taarifa hiyo.

Vilevile, TMDA imetoa wito kwa wananchi kutoa taarifa ofisi za TMDA Makao Makuu na ofisi za Kanda zilizopo Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma, Songea, Tabora na Geita au kupitia barua pepe ya info@tmda.go.tz, ofisi za afya za Halmashauri  au kupiga simu bila malipo kupitia Na.0800110084 endapo wataona dalili zozote za matumizi hayo hatari.

Chapisha Maoni

0 Maoni