Mamlaka ya
Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), imesema kwamba imepata taarifa juu ya uwepo wa
baadhi ya wafugaji wanaotumia vibaya dawa za kufubaza makali ya Virusi vya
UKIMWI (ARV's) ili kunenepesha mifugo yao.
Taarifa
iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Mkurugenzi Mkuu wa TMDA Dkt. Adam Fimbo
imesema mamlaka hiyo inakemea matumizi hayo kwani yana madhara makubwa kwa afya
ya jamii.
Imesema kuwa
dawa hizo zinatakiwa zitumike kwa ajili ya kufubaza makali ya virusi vya UKIMWI
kwa binadamu baada ya mgonjwa kushauriwa na daktari, na hivyo matumizi yake
katika kulisha mifugo kuna hatarisha afya ya jamii.
“TMDA
inaelekeza wafugaji wote wanaofanya hivyo kuacha mara moja. Aidha, Kuanzia sasa
TMDA imeanza uchunguzi wa kina katika mashamba mbalimbali ya mifugo ili kubaini
wanaojihusisha na matumizi holela ya dawa na atakayebainika kufanya hivyo,
atachukuliwa hatua kali za kisheria ikiwemo kuharibiwa kwa mifugo yake kwani
itakuwa mazao ya mifugo husika haifai tena kwa matumizi ya binadamu,” imesema
taarifa hiyo.
Vilevile,
TMDA imetoa wito kwa wananchi kutoa taarifa ofisi za TMDA Makao Makuu na ofisi
za Kanda zilizopo Dar es Salaam, Mwanza, Arusha, Mbeya, Dodoma, Songea, Tabora
na Geita au kupitia barua pepe ya info@tmda.go.tz, ofisi za afya za
Halmashauri au kupiga simu bila malipo
kupitia Na.0800110084 endapo wataona dalili zozote za matumizi hayo hatari.
0 Maoni