Shule 25 za Sekondari za wasichana za mikoa zimekamilika

 

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema Shule 25 kati ya Shule 26 za Wasichana za Sayansi za Mikoa zinazojengwa kupitia mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP) zimekamilika na zimeshapokea wanafunzi.

Hata hivyo, ujenzi wa shule iliyosalia inayojengwa Mkoa wa Morogoro upo mbioni kukamilika.

Waziri  Mchengerwa ameyasema hayo mbele ya Rais Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan alipokuwa akiweka jiwe la Msingi katika Shule ya Sekondari ya Sayansi ya Wasichana ya Mkoa wa Rukwa (Rukwa Girls) leo Julai 17, 2024 wakati wa ziara yake mkoani humo.

 "Mhe. Rais mradi huu ni ndoto zako Mhe. Rais za kwenda kuongeza ufahamu kwa watanzania na si kuongeza ufahamu pekee ila umewafikiria watoto wa kike, napenda kukujulisha kuwa Mikoa 25 imeshakamilisha ujenzi na wanafunzi wamekwisharipoti shuleni."

"Serikali imekwishatoa Shilingi Bilioni 104 kati ya Sh.Bilioni 106.6 zilizotengwa kwenye bajeti kwa ajili ya ujenzi wa Shule hizo za Sekondari za Wasichana sawa na asilimia 98 na kwa hapa Rukwa Girls wamekwishapokea Shilingi Bilioni 3 na shilingi Bilioni. 1.1 tutawaletea hivi karibuni kwa ajili ya kukamilisha miundombinu iliyobakia lakini mpaka sasa wanafunzi 157 wameripoti na kuanza masomo yako," Mhe. Mchengerwa.

Amefafanua  kuwa katika mradi huo Mhe. Rais aliidhinisha shilingi Trilioni 1.2 kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya Shule za Sekondari na mpaka sasa shule za Sekondari za Kata 402 zimeshajengwa pamoja na shule za Wasichana za Sayansi za Mikoa 25 ikiwemo ya Rukwa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akiweka jiwe la Msingi la ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Mkoa wa Rukwa kwenye hafla iliyofanyika katika Kijiji cha Mtindilo Laela mkoani humo tarehe 17 Julai, 2024.


Chapisha Maoni

0 Maoni