Kiboko wa ajabu awatesa wanavijiji, wakija askari haonekani

 

Wananchi wa Kata ya Mtipwili na Chiwanda Wilayani Nyasa wamekumbwa na taharuki baada ya Kiboko Kuvamia mashamba na kula mazao ya mihogo, mpunga na viazi katika Vijiji vya Chiulu, Kwambe, Mtipwili na Malini.

Wananchi hao wametoa kero inayowakabili, katika Mikutano ya Hadhara katika Vijiji hivyo ambapo Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mh. Peres Magiri anafanya Ziara ya Kikazi ya Kukagua Miradi ya maendeleo, Kusikiliza na kutatua kero za wananchi, kupitia Kampeni yake “Kijiji kwa Kijiji”.

Wananchi hao wamefafanua kuwa, moja ya kero inayowakabili ni uharibifu wa mazao ya chakula yanayoharibiwa na viboko ambao wapo wawili, wanaotembea pembezoni mwa Ziwa Nyasa katika kata ya Mtipwili na Chiwanda hivyo kuwapa wasiwasi mkubwa wa mazao na uhai.

Awali wametoa Taarifa Ofisi ya Maliasili na wataalam wamefika, zaidi ya mara mbili na kutofanikiwa kumuona.Hivyo Mh. Mkuu wa Wilaya tunaomba utusasaidie kutatua kero hii ili tuweze kuwa na amani. 

Diwani Viti maalum Kata ya Chiwanda,Catherine Mawila amethibitisha mbele ya Mkutano huo, ni kweli kero hii inawasumbua sana wakazi wa wa Kata ya Chiwanda na Mtipwili na kuwataka kutoa ushirikiano kwa Askari wa Mali Asili wanapofika mkatika maeneo yao.

“Ni kweli tatizo hili lipo na linawakabili wananchi wa Kata hizi mbili za Mtipwili na Chiwanda, ila wakija askari huyu kiboko haonekani na wakiondoka anaonekana sasa sisi wananchi tunatakiwa kutoa ushirikiano,” alisema Diwani Mawila.

Mkuu wa Wilaya ya Nyasa Mh. Peres Magiri amesema anaichukua kero hii na kwenda kuifanyia kazi ili kutatua changamoto hii, kwa haraka iwezekanavyo ikiwa ni pamoja na kuwataka Askari wa Maliasili kuja kukaa kwa muda mrefu ili waweze kuwaua Viboko.

Aidha, amewaagiza wananchi kufanya kazi kwa juhudi kwa kutotegemea mazao ya uvuvi pekee bali wajikite kwenye kilimo cha mahindi, maharage, soya, mbaoga mboga, na mazao mengine yanayostawi katika mazingira hayo.

Na. Netho sichali- Afisa Habari wilaya ya Nyasa

Chapisha Maoni

0 Maoni