Massana Mwishawa Naibu Kamishna mpya TANAPA

 

Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Mussa Nassoro Kuji ameongoza uapisho wa Naibu Kamishna mpya wa Uhifadhi Massana Gibril Mwishawa anayeshughulikia Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara katika Shirika la Hifadhi za Tanzania (TANAPA).

Hafla ambayo imeambatana na uvalishwaji wa cheo kipya cha Unaibu Kamishna wa Uhifadhi imefanyika Makao Makuu ya TANAPA leo jijini, Arusha.

Akitoa salamu za Pongezi baada ya Uapisho huo Kamishna Kuji alisisitiza uwajibikaji na kumtanguliza Mungu katika kutekeleza majukumu hayo ya Naibu Kamishna wa Uhifadhi.

 ”Cheo huambatana na majukumu na uwajibikaji. Hivyo basi, ni muhimu ukamtanguliza Mwenyezi Mungu wakati wote ili aweze kukuongoza katika utekelezaji wa majukumu yako haya mapya. Taaluma, uzoefu, umahiri na kujituma kwako, kunatupatia imani kubwa kuwa utatekeleza majukumu yako kwa uadilifu, weledi, bidii kubwa na bila woga wala upendeleo,” alisisitiza Kamishna Kuji.

Aidha, Kamishna Kuji aliongeza kuwa katika nafasi ya Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayeshughulikia Maendeleo ya Biashara kipaumbele cha kwanza cha Shirika ni usalama wa rasilimali za Taifa na utolewaji wa huduma bora kwa wateja wakiwemo Watalii na kusisitiza zaidi ubunifu katika mikakati endelevu katika kuinua utalii na Uhifadhi.

”Ujitahidi wakati wote kuongeza ubunifu na kuja na mikakati endelevu ambayo itainua sekta ya uhifadhi na utalii ili Shirika liweze kushiriki kikamilifu katika kumuunga mkono Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika jitihada zake za makusudi za kuinua sekta ya uhifadhi na utalii hapa nchini.”

Naye, Naibu Kamishna wa Uhifadhi Massana Gibril Mwishawa ameishukuru Bodi ya Wadhamini ya TANAPA kwa kumteua kushika nafasi hiyo ya Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara lakini pia Mhe.Dkt.Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jitihada zake za makusudi anazoendelea kuzifanya katika kuinua sekta ya uhifadhi na utalii hapa nchini.

“Mmenipa deni kubwa sana kwenu kwa watumishi wote nitakao waongoza natambua cheo nilichovishwa leo kina majukumu makubwa ambayo yananihitaji kuwajibika kikamilifu ili kukabiliana na changamoto mbalimbali za kiuhifadhi zilizopo sasa na kuimarisha uhifadhi na utalii ndani ya shirika ninaahidi nitaendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika Hifadhi zote za Taifa,” alisema Kamishna  Mwishawa.

Bodi ya Wadhamini ya TANAPA tarehe 29.04.2024 ilimteuwa Kamishna Msaidizi Mwandamizi Massana Gibril Mwishawa kuwa Naibu Kamishna wa Uhifadhi anayeshughulikia Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara, awali kabla ya uteuzi huo alikuwa Kamanda wa Uhifadhi Kanda ya Mashariki akisimamia Hifadhi ya Taifa Nyerere, Mikumi, Saadani, na Milima ya Udzungwa.

Na. Edmund Salaho/ Arusha

Chapisha Maoni

0 Maoni