Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii imesikia
kilio cha muda mrefu cha Wananchi wanaodhuriwa na Wanyama wakali na waharibifu
akiwemo Tembo kwa kuboresha viwango vya kifuta jasho na kifuta machozi kutoka
shilingi milioni moja hadi milioni mbili kwa mwananchi atakayepoteza uhai,
shilingi laki tano hadi milioni moja kwa ulemavu wa kudumu na kutoka shilingi
laki mbili hadi laki tatu kwa majeraha ya muda mfupi.
Akizungumza katika Semina ya Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania iliyoandaliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kwa ajili
ya kuwajengea uelewa wabunge hao kuhusu namna Wizara inavyoshughulikia
changamoto mbalimbali zinazosababishwa na Wanyama wakili na waharibifu Waziri
wa Maliasili na Utalii Mhe. Anjellah Kairuki amesema Serikali imefanya
maboresho ya kanuni za fidia za mwaka 2011 si kwa binadamu tu bali hata kwa
upande wa mazao ambapo kwa sasa Mwananchi atalipwa kifuta jasho cha shilingi
laki moja na nusu kutoka shilingi 37 elfu za awali kwa heka kwa kuzingatia
umbali wa shamba kutoka hifadhini.
Mhe. Kairuki amewaomba Wabunge hao kuwahamasisha watendaji
wa Halmashauri kuwasilisha wizarani kwa wakati taarifa za matukio ya mauaji,
majeruhi au uharibifu wa mashamba unaofanywa na wanyamapori walioanishwa
kisheria kulipiwa fidia ili kuwezesha mchakato wa malipo kufanyika kwa wakati
na kuondoa malalamiko ya ucheleweshaji wa malipo kwa wananchi walioathirika.
Akizungumza wakati akijibu baadhi ya hoja za Wabunge hao,
Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dastan Kitandula amesema mbali na
madhara yanayosababishwa na Tembo lakini pia Mamba ni mmojawapo ya Wanyama
wanaosababisha vifo na ulemavu kwa baadhi ya wananchi hivyo Wizara ipo katika
mchakato wa kutambua maeneo ambayo matukio ya binadamu kushambuliwa na mamba
yanajitokeza mara kwa mara hususani wakati wa kuteka maji tofauti na matukio
yanayotokea wakati wa uvuvi ili kuanzisha mfumo wa kutumia vizimba
itakayosaidia kupunguza matukio hayo.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Ardhi, Maliasili na Utalii Mhe. Timotheo Mzava amesema Wabunge wanatambua
jitihada zinazofanywa na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii kutatua
changamoto ya madhara yanayosababishwa na wanayama wakali na waharibifu na
kutaka jitihada zaidi na tafiti za kisayansi ziendelee kufanyika ili kupata
suluhu ya kudumu ya tatizo hilo.
Amesema hatua zinazochukuliwa na Wizara ya Maliasili ya
kutengeneza vifaa mbalimbali vya kufukuza Tembo ikiwemo Mabomu, mizinga ya
nyuki na utoaji wa elimu kwa kiasi kikubwa imesaidia kupunguza madhara kwa wananchi
na kuomba kutengwa kwa bajeti ya kutosha ili vifaa hivyo vitengenezwe kwa wingi
na kuwafikia wananchi wengi zaidi nchini.
Wakichangia katika Semina hiyo baadhi ya Wabunge wameomba kusogezwa kwa ukaribu huduma ya maafisa wanyamapori katika maeneo ya wananchi kwa kujenga ofisi ndogo za maafisa wanayamapori wenye vifaa na ujuzi wa kuwafukuza wanayamapori hususani Tembo pindi wanapovamia makazi na mashamba ya wananchi hususani katika maeneo yanayozunguka hifadhi za Taif ana mapori tengefu.
Na. Emmanuel Buhohela
0 Maoni