Taasisi ya Utafiti wa Wanyamapori Tanzania (TAWIRI) imepokea
vifaa vyenye thamani yaTsh. 242,000,000 kutoka Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani USAID
kupitia mradi wake wa Tuhifadhi Maliasili.
Akizungumza katika hafla ya iliyofanyikia Makao ya TAWIRI,
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya
TAWIRI Dkt. David Manyanza ameishukuru USAID kutoa vifaa ambavyo ni muhimu katika tafiti za wanyamapori hususan sensa ya wanyamapori ambayo hufanyika
kila baada ya miaka miwili hadi mitatu.
"Kama alivyowahi kusema Hayati Rais. Ali Hassan Mwinyi, mali bila daktari hupotea bila habari hivyo hatuna budi kuidadi wanyamapori ili kuwa na
uhifadhi endelevu wa wanyamapori hapa chini,” ameeleza Dkt. Manyanza.
Dkt. Manyanza amesema vifaa hivyo vina mchango mkubwa kwenye
sekta ya Maliasili kwani tafiti za TAWIRI zinasaidia kuzishauri mamlaka za uhifadhi, "Nitoe wito kwa wadau kujitokeza kushirikiana na
TAWIRI ili kuwezesha tafiti za wanyamapori kwa ustawi wa uhifadhi na
kukuza utalii, " ameeleza Dkt. Manyanza.
Kiongozi wa Idara ya mazingira na usimamizi wa Maliasili
kutoka Shirika la Maendeleo la Kimataifa la Marekani (USAID), Nathan Sage,
amesema kwa miaka 60 sasa, USAID imekuwa ikishirikiana Tanzania kuhifadhi
bioanuwai ikizingatiwa Tanzania ina
utajiri mkubwa wa rasilimali za
kibaolojia ikiwemo maliasili ya Wanyamapori
ambao wana thamani kubwa ya kitamaduni, kiuchumi na kielimu.
Aidha, Bw. Sage amesema katika kuendeleza ushirikiano huo,
USAID imetoa vifaa vyenye thamani ya
Shilingi Milioni 242 kwa TAWIRI ili kuimarisha uhifadhi kwa kuwezesha matumizi
ya teknolojia kurahisisha tafiti za wanyamapori.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu TAWIRI Dkt. Eblate Mjingo amesema Jukumu kuu la
TAWIRI ni kufanya tafiti za wanyamapori ambapo ameishukuru USAID kutoa vifaa
ambavyo ni Kamera za kufunga kwenye ndege wakati wa kuidadi wanyamapori,
Mikanda ya visukuma mawimbi ya Tembo (GPS Collars) na Vifaa vya Majira nukta (Location GPS).
"Utafiti ni
gharama, unahitaji vifaa na teknolojia, hivyo vifaa hivi tulivyopokea
vinakwenda kusaidia sana hususani kwenye sensa ya wanyamapori.
0 Maoni