Zoezi la ubomoaji wa nyumba zilizofidiwa na Mradi wa
Uendelezaji wa Bonde la Msimbazi linatarajiwa kuanza rasmi Aprili 12, 2024, na
litawahusu waathirika 2,155 ambao tayari wamelipwa fidia.
Hayo yamesemwa leo tarehe 25 Machi, 2024 na Mhandisi Humphrey
Kanyenye, Mratibu wa Miradi ya Ushirikiano na Benki ya Dunia TARURA alipokuwa
akiongea na waandishi wa habari katika ofisi za mradi zilizopo Millenium
Tower-Kijitonyama, Dar es Salaam.
Mhadisi Kanyenye alieleza kuwa kwa mujibu wa makubaliano ya
utekelezaji wa zoezi hilo, waathirika wa mradi ambao wameshakwishapokea malipo
yao wanatakiwa kuhamisha mali zao na kupisha eneo la mradi ndani ya wiki sita
(6) baada ya kupokea fedha hizo kwenye akaunti zao.
“Waathrika wote wa mradi huu wanafahamu kuwa tuliwapa muda wa
kuhama kwa makubaliano maalumu ya kimkataba yaliyowataka kuhama ndani ya wiki
Sita (6) mara tu baada ya fedha kuingia katika akaunti zao, muda huo sasa
umepita hivyo wanatakiwa kuondoka ili kupisha utekelezaji wa mradi,” alisema
Mhandisi Kanyenye.
Alieleza pia kuwa walichelewa kuanza zoezi hilo kwa ajili ya
kuwapa muda waathirika wa mradi kubomoa wenyewe kwa hiari ili kuokoa baadhi ya
mali zao.
Aidha, alisema kwamba
kati ya waathirika 2,329 waliopo kwenye orodha ya daftari la kwanza la
ulipaji fidia, kufikia tarehe 21 Machi 2024, tayari waathirika 2,151 walikuwa
wamelipwa kiasi cha shilingi bilioni 52.6
“Lakini pia kuna wale ambao hawakufikiwa katika uthamini wa
awali kwa baadhi yao kugomea ama kutoonekana katika maeneo yao, idadi yao ni
466, hawa wameingizwa katika orodha ya daftari la pili ambalo limeshakamilika
na litawasilishwa kwa Mthamini Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kusainiwa siku ya
jumanne tarehe 26 Machi 2024 tayari kwa kulipwa fidia,” alisema Mhandisi
Kanyeye.
Mradi unatekelezwa kwa muda wa miaka sita (6) (2022-2028) kwa
gharama takribani shilingi bilioni 663 na lengo kuu la mradi ni kuimarisha
ustahimilivu kwa kuweka mikakati ya kukabiliana na mafuriko na kuwa na matumizi
bora ya ardhi katika eneo la chini la bonde la mto msimbazi ikiwa ni pamoja na
kurudisha uoto wa asili katika uwanda wa juu wa bonde la Mto Msimbazi.
0 Maoni