Sekta ya Utalii yaongoza kuingiza fedha za kigeni nchini

 

Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) na Msemaji Mkuu wa Serikali Bw. Mobhare Matinyi amesema Sekta ya Utalii ndiyo sekta inayoongoza hivi sasa kwa kuiletea nchi fedha za kigeni.

Akiongea leo Dar es Salaam na Wahariri na Waandishi wa Habari wakati akielezea mafanikio ya miaka mitatu ya Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, Bw. Matinyi amesema mapato ya utalii sasa yamefikia dola za Marekani bilioni 3.37 (zaidi ya shilingi trilioni 8).

Kimsingi sekta hii imemrejeshea shukurani Mhe. Rais Samia kwa juhudi zake binafsi za kutoka ofisini na kwenda kushiriki katika utengenezaji wa filamu ya “Tanzania: The Royal Tour”, amesema Bw. Matinyi.

Amesema kuwa katika kipindi cha miaka mitatu idadi ya watalii nchini imeongezeka kutoka 922,692 mwaka 2021 walioipatia nchi mapato dola za Marekani bilioni 1.31 hadi watalii 1,808,205 mwaka 2023 walioingiza dola bilioni 3.37.

Ameeleza kwamba kwa kuongeza idadi ya watalii wengi baada ya mlipuko wa UVIKO-19 Tanzania sasa inashika nafasi ya pili barani Afrika baada ya Ethiopia; na kwa kuongeza mapato makubwa inashika nafasi ya tatu baada ya Moroko na Morisi (Mauritius).

“Tanzania imeendelea kutambuliwa kimataifa na kupata tuzo mbalimbali. Tuzo hizo ni Hifadhi ya Taifa Serengeti kuwa hifadhi bora barani Afrika kwa miaka mitano mfululizo kuanzia mwaka 2019 hadi 2023,” amesema Bw. Matinyi.

Pia, amesema Tanzania kuwa nchi ya saba miongoni mwa nchi 18 duniani zilizo bora kutembelewa kiutalii kwa mwaka 2022, ambapo Hifadhi ya Taifa Serengeti kuorodheshwa kama eneo maridhawa la kutembelewa kwa mwaka 2023 na Hifadhi ya Taifa Serengeti kushika nafasi ya tatu ya vivutio bora vya asili duniani kwa mwaka 2023.

Aidha, Bw. Matinyi amesema Mamlaka ya Eneo la Hifadhi ya Ngorongoro imeshinda tuzo mbili za Best of the Best Travelers’ Choice na Africa’s Leading Tourist Destination kwa mwaka 2023. Hizi ni baadhi ya tuzo ambazo Tanzania imezipata kimataifa; si zote.

Chapisha Maoni

0 Maoni