NCAA yapokea gari ya kutatua migogoro kati ya binadamu na wanyamapori

 

Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongro (NCAA) imepokea gari aina ya Suzuki Jimny kutoka shirika lisilo la kiserikali la Elephant Protection Initiative (EPI) ya nchini Uingereza kupitia mbia wake Kampuni ya ulinzi ya GardaWorld Tanzania kwa lengo la kusaidia kupunguza Migogoro kati ya wanyamapori na wananchi.

Akipokea gari hiyo kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi NCAA, kaimu meneja wa huduma za Ulinzi NCAA SCO Donatus Gadiye ameeleza kuwa gari hiyo imetolewa kwa ajili kuimarisha ulinzi na kupunguza migogoro kati ya wanyamapori na wananchi wanaozunguka hifadhi ya Ngorongoro hasa kwa wanyama wakali kama tembo kuvamia mashamba ya wananchi.

"Gari hili linabeba askari wanne kwa pamoja na lina uwezo wa kupita kwenye matope na barabara ngumu ikiwemo zinazotenganisha mpaka wa hifadhi na mashamba ya wananchi na kusaidia kutatua changamoto hizo kwa haraka," ameeleza Gadiye.

Gadiye ameongeza kuwa askari wa jeshi la Uhifadhi watakaotumia gari hilo watakuwa na uwezo wa haraka kusoma tabia za tembo hasa wanaoingia maeneo ya wananchi na kubuni njia za kupambana nao kwa haraka.

Mkurugenzi wa GardWorld tawi la Tanzania Tommy Bright ameeleza kuwa taasisi yao imekuwa ikisaidia miradi mbalimbali inayolenga ulinzi wa Wanyamapori kwa ajili ya kupunguza migogoro kati ya Wanyamapori na binadamu na kuangalia njia mbalimbali za kisasa katika kupambana na hali hiyo.



Chapisha Maoni

0 Maoni