Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongro (NCAA) imepokea gari aina ya
Suzuki Jimny kutoka shirika lisilo la kiserikali la Elephant Protection
Initiative (EPI) ya nchini Uingereza kupitia mbia wake Kampuni ya ulinzi ya
GardaWorld Tanzania kwa lengo la kusaidia kupunguza Migogoro kati ya
wanyamapori na wananchi.
Akipokea gari hiyo kwa
niaba ya Kamishna wa Uhifadhi NCAA, kaimu meneja wa huduma za Ulinzi NCAA SCO
Donatus Gadiye ameeleza kuwa gari hiyo imetolewa kwa ajili kuimarisha ulinzi na
kupunguza migogoro kati ya wanyamapori na wananchi wanaozunguka hifadhi ya
Ngorongoro hasa kwa wanyama wakali kama tembo kuvamia mashamba ya wananchi.
"Gari hili linabeba askari wanne kwa pamoja na lina
uwezo wa kupita kwenye matope na barabara ngumu ikiwemo zinazotenganisha mpaka
wa hifadhi na mashamba ya wananchi na kusaidia kutatua changamoto hizo kwa
haraka," ameeleza Gadiye.
Gadiye ameongeza kuwa askari wa jeshi la Uhifadhi watakaotumia
gari hilo watakuwa na uwezo wa haraka kusoma tabia za tembo hasa wanaoingia
maeneo ya wananchi na kubuni njia za kupambana nao kwa haraka.
Mkurugenzi wa GardWorld tawi la Tanzania Tommy Bright ameeleza
kuwa taasisi yao imekuwa ikisaidia miradi mbalimbali inayolenga ulinzi wa
Wanyamapori kwa ajili ya kupunguza migogoro kati ya Wanyamapori na binadamu na
kuangalia njia mbalimbali za kisasa katika kupambana na hali hiyo.
0 Maoni