WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali imeridhia kutoa
sh. bilioni 1.3 ili kukamilisha soko la kimataifa la mazao ya kilimo
lililopo Renagwe, wilayani Tarime, mkoani Mara.
“Masoko haya tumeyajenga kila palipo na mpaka. Tumejenga
Namanga, Tunduma, Kasumulo, Horohoro, Holili pamoja na hili la Tarime ambalo ni
la muda mrefu, zabuni ya kulikamilisha hili na la Horohoro tayari
zimeshatangazwa,” amesema.
Ametoa kauli hiyo leo
(Jumatano, Februari 28, 2024) wakati akizungumza na mamia ya wakazi wa Sirari
kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika uwanja wa Tarafa, wilayani Tarime,
mkoani Mara.
Waziri Mkuu amesema kuwa zabuni zimekwishatangazwa na kazi itaanza
kabla mwezi Machi haujaisha. “Serikali inataka wakulima walitumie soko hilo
kupeleka mazao yao ili wanunuzi kutoka ndani na nje ya nchi wakanunue mazao
katika soko hilo.”
Ametumia mkutano huo kuwaagiza mameneja wa TANESCO katika
mikoa na wilaya nchini wapige kambi vijijini na kutoa huduma hapohapo ili
kurahisisha ulipaji wa gharama za kuunganishiwa umeme badala ya kusubiri
kufuatwa makao makuu.
Wakati huohuo, Waziri Mkuu amesema watumishi wa umma
wanapaswa kuweka ratiba ya kuwatembelea wananchi walioko vijijini ili
wawasikilize na kuwapatia ufumbuzi wa matatizo waliyonayo.
“Hapa nimepokea hoja kwenye mabango na Rorya pia niliyaona
mabango. Hii ni dalili kuwa watu wana kero zao lakini hawana majibu. Watumishi
wa umma mnatakiwa kila siku muwe na ratiba ya kuwatembelea wananchi kwenye
maeneo yao, mkae kwa utulivu na kusikiliza hoja zao. Pia mchukue hoja hizo na
kuzipatia majibu hukohuko, wananchi wasisumbuke kuja kuwafuata ofisini,”
amesisitiza.
Waziri Mkuu amesisitiza kuwa: “Masuala mengi yanayoelezwa
kwenye haya mabango ni ya kiutendaji, yanawahusu ninyi na ndiyo maana nimekuwa
nasisistiza kuwa kati ya siku sita za kazi, mtenge siku tatu hadi nne, mpite
vijijini kusikiliza kero za wananchi na kuzitatua.”
CHANZO: Ofisi ya Waziri Mkuu
0 Maoni