Ziara ya maafisa wa TANAPA yakonga mioyo ya mawakala wa utalii Zanzibar

 

Ziara zinayofanywa na Maafisa kutoka Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) wanaoshiriki Maonesho ya 10 ya Biashara ya Kimataifa Fumba - Zanzibar ya kuwatembelea Wadau wa utalii na Mawakala wa usafirishaji wa anga (ndege) imeleta matumaini mapya yatakayochagiza ongezeko la wataii ndani ya Hifadhi za Taifa, hasa upande wa Kusini unaopokea watalii wengi kutoka Zanzibar na kuimarisha ushirikiano baina ya wadau hao na TANAPA.

Akiongea kwa furaha na matumaini makubwa, Mkurugenzi wa Ndonga Adventure Bw. Abuu Bakari Abdallah alisema, "Nimefarijika sana kuja kwenu na kufanya mazungumzo nami, nimegundua kuwa mnathamini mchango wangu wa kuleta wageni katika Hifadhi za Taifa zilizoko Mashariki na Kusini mwa Tanzania. Wageni wangu huridhishwa sana na huduma nzuri zinazotolewa Mikumi na Nyerere na wamekuwa wakitoa au kuandika (comments) nzuri, niwapongeze sana kwa kazi na huduma nzuri mnazotoa kwa watalii".

Aidha, Mkurugenzi huyo aliongeza kuwa "Nimekuwa nikipata ushirikiano mzuri kutoka TANAPA hata ninapopata tatizo hifadhini maafisa na askari wenu huwa pamoja nasi hadi mwisho wa tatizo na kuna wakati watakusubiri hadi wajue wewe na wageni wako mtalala wapi ndio waendelee na majukumu yao."

Naye, Mwakilishi wa Auric Air Zanzibar - Bi. Hajra Hazaa, aliwashuru TANAPA kwa ujio wao katika Ofisi za Auric Air zilizopo katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Zanzibar na kuliomba Shirika hilo lenye Makao Makuu yake jijini Arusha kuboresha miundombinu ya barabara na Viwanja vya ndege.

Afisa Mwandamizi anayeshughulikia masuala ya Utalii Hifadhi Taifa Mikumi - Herman Baltazary, aliwahakikishia wadau hao maboresho makubwa ya ujenzi wa barabara na Viwanja vya ndege yanayofanyika ndani ya Hifadhi za Taifa Mikumi, Ruaha na Nyerere inayotekelezwa kupitia Mradi wa REGROW.

"Nikushauri pia kutumia Kiwanja cha Ndege cha Msolwa ili wageni wenu waweze kulala na kupata nafasi ya kutembelea Hifadhi za Taifa Udzungwa kwa ajili ya kupanda mlima na kujionea Maporomoko ya Sanje, Mikumi na Ruaha kuangalia wanyama na nyika tofauti bila kuisahau Nyerere kwa ajili ya "boat safari". Kwa kufanya hivyo wageni wenu watakuwa wamepata vionyo na radha tofauti ya utalii," aliongeza mwandamizi huyo.

Ziara ya Maafisa kutoka TANAPA kuwatembelea wadau wa utalii ilianza takribani siku nne zilizopita na leo tarehe 16.01.2024 imendelea katika viunga na ofisi mbalimbali za wadau wa utalii na mawakala wa usafirishaji walioko Zanzibar.

Na. Jacob Kasiri- Zanzibar

Chapisha Maoni

0 Maoni