Taratibu hazijakiukwa mamba mkubwa aliyewindwa- TAWA

MWENDELEZO WA TAARIFA KUHUSU KUSAMBAA KWA PICHA JONGEFU (VIDEO CLIP) INAYOONYESHA MWINDAJI AKIWA NA MAMBA ALIYEWINDWA

Itakumbukwa kuwa tarehe 27/12/2023, Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) ilitoa taarifa ya awali kwa umma kuhusu suala hili na kuahidi kufanya uchunguzi zaidi.

TAWA inapenda kuufahamisha umma kuwa uchunguzi kuhusu suala hili umekamilika. Hivyo, taarifa ifuatayo inatoa ufafanuzi kuhusu uwindaji wa mamba husika na dhana nzima ya uwindaji nchini na duniani.

Shughuli za uwindaii ikiwemo wa mamba nchini zipo kisheria zikisimamiwa na Sheria za ndani na za kimataifa kupitia Mkataba wa Kimataifa wa biashara ya wanyamapori na mimea iliyohatarini kutoweka (Convention on International Trade in Endangered Species of Wild Fauna and Flora - CITES).

Kwa mujibu wa taratibu za mkataba wa kimataifa wa CITES, Tanzania imeruhusiwa kuwinda mamba wasiozidi 1,600 kwa mwaka. Mpaka sasa jumla ya mamba 39 tu kati ya 1,600 wamewindwa kutoka kwenye mgawo (quota) wa Taifa wa mwaka 2023.

Mamba anayeonekana kwenye picha jongefu (video clip) iliyosambaa aliwindwa katika kitalu cha Lake Rukwa GR kwa kibali halali namba MP-0001792 kilichoanza tarehe 12/08/2023 hadi 09/09/2023.

Mamba huyo alikuwa na urefu wa futi 16.2 sawa na sentimita 493.8 ikiwa ni juu ya kiwango cha chini cha urefu wa sentimita 300 unaohitajika kwa mujibu wa Sheria. Aidha, kwa mujibu wa takwimu za taasisi ya Marekani (Safari Club International - SCI), mamba mrefu zaidi duniani aliwindwa nchini Ethiopia mwaka 2005 (futi 18.7 sawa na sentimita 561).

Vilevile, kumbukumbu zinaonesha, uwindaji huu ulisimamiwa na askari kutoka TAWA na mwindaji bingwa kutoka kwenye kampuni iliyopewa kibali kwa mujibu wa Sheria.  Aidha, ada na tozo zote zinazohusiana na uwindaji wa mamba zililipwa kwa kuzingatia Sheria na Kanuni zinazosimamia uwindaji hapa nchini.

Wakati uwindaji ukifanyika askari anayesimamia uwindaji uhakikisha uwindaji unafanyika kwa kuzingatia Sheria na kulinda usalama wa wageni wawindaji na watu walioambatana nao. Hivyo taratibu zote hizi za kisheria zilizingatiwa na hakuna utaratibu uliokiukwa.

Kwa taarifa hii, umma unahakikishiwa kuwa uwindaji wa wanyamapori nchini unazingatia Sheria na taratibu za ndani ya nchi na zile za kimataifa na Mamlaka inawatoa hofu kuwa taratibu hizi zinasimamiwa ipasavyo na pale panapotokea ukiukwaji hatua stahiki huchukuliwa kwa mujibu wa Sheria.

Mamlaka inawashukuru watanzania wote waliopaza sauti zao wakionesha utayari wa kulinda rasilimali zetu na kutaka kujiridhisha kuhusu uhalali wa uwindaji husika.

Imetolewa na:                                                                                                  

 

                                                       Beatus Maganja

                                                      AFISA HABARI

                            KITENGO CHA UHUSIANO KWA UMMA - TAWA


Chapisha Maoni

0 Maoni