Waliokufa kwa maporomoko ya matope Hanang wafikia 85

 

Taarifa ya Serikali kuhusiana na maendeleo na hali baada ya kutokea maafa wilayani Hanang mkoani Manyara imeeleza kuwa hadi kufikia sasa miili iliyopatikana ni 85 na yote imeshatambuliwa na ndugu zao na kuchukuliwa.

Taarifa hiyo iliyotolewa leo wilayani Hanang na Msemaji Mkuu wa Serikali Mobhare Matinyi imesema idadi hiyo ya vifo ipo katika mchanganuo ambao watu wazima ni 49 (wanaume 20 na wanawake 29), na watoto 36 (kiume 16 na kike 20).

Taarifa hiyo imeongeza kwamba hadi sasa jumla ya majeruhi na wagonjwa waliopokelewa tangu maafa ya maporomoko ya matope kutoka MlimaHanang yatokee ni 139 lakini waliopo hospitalini ni 51.

Aidha, taarifa hiyo imesema kutokana na juhudi za Serikali za kuwapa ushauri nasaha, kuwasaidia kupata mahitaji muhimu na chakula pamoja na kuwaunganisha na ndugu na jamaa zao, waathirika kwenye kambi wamepungua kutoka 440 hadi 322.

Serikali inaendelea kuwashukuru na kuwapongeza Watanzania pamoja na taasisi za umma na binafsi za ndani ya nchi yetu kwa moyo wa utu na uzalendo. Serikali inatoa wito kwa wanaojitolea kufanya hivyo kwa kuleta vifaa vya ujenzi ili visaidie kuwapatia makazi mapya waathirika wa maafa haya, imesema taarifa hiyo.

Chapisha Maoni

0 Maoni