WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amevitaka vyuo vinavyotoa elimu
kuhusu masuala ya Ustawi wa Jamii nchini vifanye mapitio ya mitaala ili iendane
na wakati na itoe majibu kwa changamoto za sasa za jamii sambamba na kufanya
tafiti mbalimbali ikiwemo tafiti za masuala ya malezi na maadili.
Amesema Serikali ya awamu ya sita kwa upande wake itaendelea
kutekeleza azma yake ya kuimarisha ustawi wa wananchi kwa kuendelea kufanya
maboresho ya mifumo, ufuatiliaji na usimamizi wa masuala ya ustawi wa jamii
sambamba na kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya utekelezaji wa afua
mbalimbali.
Ametoa agizo hilo leo (Jumatatu, Desemba 18, 2023) kwenye
kilele cha Wiki ya Ustawi wa Jamii na Maadhimisho ya Miaka 50 ya Chuo cha
Ustawi wa Jamii, ukumbi wa JNICC - Dar es Salaam. Amesema ipo haja ya kufanya
tathmini ya mfumo mzima wa malezi na makuzi ya watoto na vijana ambayo ndio
msingi mkuu wa kukuza maadili katika jamii.
”Wazazi, walezi na Watanzania kwa ujumla kila mmoja ashiriki
katika kulinda haki na ustawi wa watoto wetu. Hii ni nguvukazi ya Taifa letu
hivyo basi, ulinzi na usalama wa watoto ni jukumu letu sote. Pia Wizara
ikamilishe programu ya ulinzi wa kijamii (social protection application) ili
ianze kutumika.”
Akizungumzia kuhusu kauli mbiu ya maadhimisho inayosema
’Malezi na Makuzi kwa Watoto na Vijana kwa Maendeleo ya Taifa’ ambayo
itaambatana na mjadala wa kitaifa unaoakisi mada hiyo, Waziri Mkuu amesema mada
hiyo ni thabiti na imekuja katika wakati muafaka.
”Nchi yetu kama zilivyo nchi nyingine duniani inapitia
changamoto ya ongezeko la vitendo vya mmomonyoko wa maadili unaochangiwa na
mitindo ya maisha. Hakuna shaka kuwa mjadala huu utawezesha kupata uelewa wa
pamoja kama Taifa ili kuweka mikakati ya kitaifa ya kukabiliana na changamoto
ya mmomonyoko wa maadili.”
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa amesema kutokana na changamoto za
kiuchumi familia nyingi zinashindwa kupata muda wa kutosha kulea watoto na
vijana ambao ni muhimu katika ujenzi wa Taifa la sasa na baadaye, hivyo mada
hiyo ni kengele ya amshaamsha kwa kila mtendaji na mwanajamii kutambua kuwa
suala la malezi na makuzi ya watoto na vijana ni msingi wa maendeleo ya Taifa
letu.
Vilevile, Waziri Mkuu amesema Maafisa Ustawi wa Jamii ni
wasuluhishi wa migogoro ya ndoa na familia, hivyo amewataka waongeze kasi ya
kutoa huduma. ”Hivi karibuni kumekuwa na changamoto kubwa ya kuvunjika ndoa na
kusababishwa ombwe katika malezi ya watoto. Tusaidieni kuimarisha taasisi ya
familia ili watoto wapate malezi bora ya wazazi wote wawili.”
Waziri Mkuu amesema pasipo misingi bora ya malezi ya watoto
na vijana Taifa halitaweza kupata ustawi bora wa jamii kama inavyotarajiwa,
ambapo ametumia fursa hiyo kukumbusha wajibu wa taasisi zote zinazohusika na
malezi ambazo ni familia, shule, madhehebu ya dini na jamii kwa ujumla kuweka
kipaumbele katika suala la malezi na makuzi ya watoto na vijana ili waweze
kujenga jamii wanayoitaka katika misingi ya uchumi, imani na uhusiano.
Kadhalika, Waziri Mkuu amesema Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM mwaka 2020 – 2025 chini ya Ibara za 89 hadi 92 imebainisha kuwa kuinua na kuimarisha maisha ya mtu, familia na makundi yenye mahitaji maalum katika jamii iwe ni nyenzo muhimu kwa mustakabali wa maendeleo endelevu na jumuishi.
Waziri Mkuu amesema upatikanaji wa huduma za ustawi wa jamii ni kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Sita na sote tumeshuhudia dhamira ya dhati ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kuyawezesha makundi yenye uhitaji, kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo na kijamii.
0 Maoni