AGRA inavyosaidia azma ya Serikali ya Tanzania kuilisha dunia

 

Ili Serikali ya awamu ya sita itimize azma yake ya Tanzania kuilisha dunia, wadau mbalimbali wa sekta ya kilimo wanamchango mkubwa katika kufanikisha azma hiyo, pamoja na Serikali kuwa na mipango thabiti ya matumizi ya mbegu zilizoboreshwa na teknolojia ya kisasa katika kilimo.

Katika kilimo mbegu ni muhimu kutokana na ukweli kwamba mbegu ni chanzo cha uhai, ni chanzo cha nishati, chanzo cha chakula na dawa, pia mbegu ni chanzo cha malighafi za viwandani na vilevile ni chanzo cha mapato ya fedha za kigeni.

Katika kuzingatia suala la mbegu ni muhimu kuwa na mbegu zilizoboreshwa ili kupata mavuno ya kutosha na kukabiliana na magonjwa, wadudu waharibifu, ukame, magungu pamoja na changamoto zingine za mazingira yakiwamo mabadiliko ya tabia nchi.

Serikali katika kutambua umuhimu wa mbegu zilizoboreshwa hadi sasa nchini kuna Wakala wa Mbegu za Kilomo (ASA), inayohusika na utafiti, ubunifu, pia uzalishaji mbegu nchini.

Pia kuna Taasisi ya Kudhibiti Ubora wa Mbegu (TOSCI) iliyoanzishwa mwaka 2003, ikiwa na jukumu la kuthibitisha na kukuza mbegu bora zinazozalishwa nchini ama kuingizwa kutoka nje ya nchi kwa ajili ya kuuzwa.

Katika kutambua umuhimu wa kilimo kwa bara la Afrika aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Hayati Kofi Annan alianzisha Taasisi inayojishughulisha na ukuzaji wa kilimo Afrika (AGRA) mwaka 2006, ili kuboresha maisha ya wakulima wadogo wa Afrika wanaohangaika na kilimo cha kujikimu na kuwafanya walime kilimo cha biashara.

Maono hayo ya Muasisi wa AGRA Hayati Annan, yameigusa Tanzania kupitia taasisi hiyo iliyopo kwenye mataifa kadhaa ya Afrika, ikishirikiana na Serikali, Wadau wa kilimo na Wakulima katika kuhamasisha kilimo cha kisasa, matumizi ya mbegu zilizoboreshwa pamoja na kuwa na soko la chakula lenye ushindani Afrika.

Afisa wa Programu ya Mifumo ya Mbegu AGRA, Ipyana Mwakasaka amesema taasisi hiyo imesaidia katika kuwawezesha watafiti nchini kubuni na kuja na aina mbalimbali za mbegu karibu 44 za mazao mbalimbali kama vile mahindi, mpunga, maharage soya, mihogo na mengineyo.

“Kati ya mbegu hizo 44 ambazo AGRA imewasaidia watafiti kufanya tafiti na kubuni mbegu, aina 30 ya mbegu hizo zimeshaingia sokoni baada ya kuidhinishwa na waziri mwenye dhamana ya kilimo, na zinafanyakazi vizuri katika mikoa mbalimbali,” alisema Bw. Mwakasaka.

Amesema kwamba AGRA pia imesaidia kuanzisha na kuyaimarisha makampuni 15 ya mbegu ya ndani ya nchi, katika kusaidia mkakati wa Serikali wa kuzalisha asilimia 75 ya mbegu nchini ili kuepukana na athari za kutegemea mbegu kutoka nje ya nchi.

“Kampuni hizo binafsi 15 za uzalisahji mbegu zilizopata msaada wa AGRA zimefanikiwa kuzalisha mbegu zenye ubora wa hali ya juu zinazofikia ujazo wa tani mitamraba 35,000,” alisema Bw. Mwakasaka na kuongeza “Uzalishaji wa mbegu bora umeongezeka kutoka tani 36,614 mwaka 2015 hadi kufikia tani 71,000 mwaka 2020.”

Bw. Mwakasaka amesema kwamba kumekuwapo pia na mafanikio ya kuongezeka kwa uzalishaji wa mbegu nchini kutoka chini ya asilimia 20 mwaka 2006 hadi kufikia uzalishaji wa mbegu unaozidi zaidi ya asilimia 60 kwa sasa.

Katika kukabiliana na upungufu wa Maafisa Ugani, AGRA imetoa mafunzo kwa wakulima viongozi 5000 wanaowahudumia wakulima wapatao 100-200, kwa kusaidiana na Maafisa Ugani Kata katika kupeleka taarifa za kilimo kwa wakulima.

AGRA pia inahusika katika kusaidia sera za pamoja na mazingira bora ya kilimo nchini kwa kufanikisha kuandikishwa Serikalini kwa mbegu za aina mbalimbali zilizoboreshwa pamoja na kuondoa ada ya uandikishaji.

Licha ya mafanikio hayo bado Tanzania inakabiliwa na changamoto ya upungufu wa mbegu zilizoboreshwa, pamoja na kuzalisha asilimia 60, kuna asilimia 40 nchi inaagiza nje ya nchi hususan kwenye mbegu za mahindi, lakini kwenye mazao mengine ni zaidi ya asilimia 90.

Changamoto hiyo pia inaeelezwa na Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Wafanyabiashara ya Mbegu Tanzania (TASTA), Bw. Bob Baldwin Shuma ambaye amesema asilimia kubwa ya mbegu za hybrid zinazotumika nchini zinazalishwa kutoka nje ya nchi.

“Mbegu zote za hybrid zinazoletwa kutoka nje haziji tu na wala sio msaada, bali zinanunuliwa kwa fedha za kigeni ndipo mnunuzi aende kununua kama ni Zimbabwe ama Zambia,” alisema Bw. Shuma na kuongeza, “Bado inatakiwa kulipa kodi kadhaa na ndio maana zinauzwa bei ghali, lakini kwa mfano sasa kunauhaba wa dola tafsiri yake ni nini tutakapo kosa dola mbegu zitakosekana, kama hatuzalishi mbegu sisi wenyewe za kutosha kunahatari”.

Amesema amekuwa akijitahidi sana kusaidia kuhakikisha kunakuwa na Sera nzuri, kwani ardhi zipo tena safi, kwa mfano maeneo yatakayotengwa kwa irrigation (kilimo cha umwagiliaji) mbegu za hybrid zizalishwe huko huko.

“Tuna mabonde mazuri ambayo yamezungumzwa yapo, hayo mabonde mimi nina nia ya kuyataja tuyafanya yawe chini ya Serikali lakini yatolewe kwa ajili ya kuzalishia mbegu za hybrid kwa njia ya umwagiliaji,” alisema Bw. Shuma.

Ameeleza kwamba ili kuzalisha mbegu za hybrid sheria ya TOSCI inasema kuzalisha mbegu hizo unatakiwa kuwa na nafasi ya mita 400 huku na mita 400 huku na mtu mwingine asilime mahindi katika eneo hilo.

“Kwa hiyo ardhi tulionayo lazima tuwe za Sera nzuri, kule tunapoenda kununua mbegu za hybrid wamefanya hivyo, sisi tusipofanya hivyo tutaendelea kununua huko mbegu hizo,” alisema Bw. Shuma.

Pamoja na changamoto za upungufu wa mbegu mabadiliko ya tabia nchi nayo yameelezwa kuwa yamekuwa yakichangia kuangamiza mbegu nyingi za asili nchini, kutokana na mbegu hizo kushindwa kuhimili changamoto zinazotokana na mabadiliko hayo.

Akiongelea suala hilo Afisa wa Taasisi ya Agri experience Dk. Emmarold Mneney, ameelezea changamoto za mabadiliko ya tabia nchi yanayopelekea kutokea kwa ukame, mafuriko, joto kali, kuibuka kwa magonjwa mapya na wadudu wapya yanavyoathiri mbegu za asili.

“Kumekuwa na dhana potofu kuwa mbegu zilizoboreshwa zinatumika kupoteza mbegu za asili, ukweli ni kwamba mbegu za asili zinaathiriwa na mabadiliko ya tabia nchi,” alisema Dk. Mneney na kuongeza “Mbegu nyingi za asili zinashindwa kuhimili hali ya mafuriko, mvua chache pamoja na joto kali, hapo ndipo mbegu zilizoboreshwa zinapokuja kusaidia”.

Dk. Mneney amesema wanachofanya watafiki wanaozalisha mbegu zilizoboreshwa ni kurudi katika mbegu za asili kuzizidishia nguvu ili ziweze kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabia nchi.

Akielezea historia ya tafiti za mbegu duniani, Dk. Mneney amesema utafiti ndio uliosaidia kupatikana kwa mbegu ya mahindi, kutoka kwenye Mexican grass (majani ya Mexico) na kuboreshwa kuwa mahindi tunayokula leo.

“Leo tusinge kuwa tunakula mahindi kusinge kuwa na utafiti wa mbegu, kwani mahindi yemetokana na tafiti iliyofanywa kutoka kwenye Mexican grass (majani ya Mexico) kwenye karne ya 16,” alisema Dk. Mneney.

Dk. Mneney amesema mbegu zilizoboreshwa ni ufumbuzi ambao utaendelea kuwapo duniani katika kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi pamoja na kuboresha uzalishaji wa mazao ili kuendana na wakati.

Pamoja na mambo mengine, Dk. Mneney amesema mafanikio ya azma ya Tanzania kuilisha dunia yatafikiwa iwapo tu Serikali itaongeza bajeti ya kilimo na kuwekeza zaidi kwenye tafiti za uzalishaji wa mbegu zilizoboreshwa.

Chapisha Maoni

0 Maoni