Kamati ya Kudumu ya Bunge ya
Nishati na Madini imewasili Jijini New Delhi, nchini India kwa ziara ya kikazi
na kujifunza namna Serikali ya India ilivyopiga hatua katika matumizi ya Gesi
Asilia (CNG na LNG), Nishati Safi ya Kupikia na Uzalishaji wa Umeme kwa kutumia
Makaa ya Mawe.
Ziara hiyo inaongozwa na
Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Judith Kapinga, kwa upande wa Serikali, ambapo
pamoja na mambo mengine, amesema kuwa kamati hiyo itajifunza masuala mbalimbali
kuhusu Sekta ya Nishati, Ushirikiano uliopo miongoni mwa wadau pamoja na jitihada
zianazofanywa na Serikali ya India katika kuongeza matumizi ya Nishati Safi ya
Kupikia.
Mhe. Kapinga amesema kuwa,
Ziara hiyo ya siku 7 kuanzia tarehe 19 hadi 24 Novemba, 2023 imelenga kutoa
mafunzo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Sekta ya
Nishati hasa katika masuala ya Nishati ya Gesi Asilia na uzalishaji wa Umeme
kwa kutumia Mkaa ya Mawe.
Alifafanua kuwa Kamati
inatembelea makampuni na viwanda mbalimbali, ambapo tayari imetembelea Kampuni
ya Mafuta ya India (Indian Oil) inayoendesha Kiwanda cha Kujaza Gesi Asilia
(Liquidfied Natural Gas – LPG), kilichopo katika Mji wa Dehli.
Naye Kaimu Mwenyekiti wa
Kamati hiyo Mhe. Kilumbe Ng’enda ameipongeza Wizara ya Nishati kwa kuandaa na
kuwezesha ziara hiyo hasa kipindi hiki ambacho nchi yetu ipo katika mipango na
mikakati madhubiti ya kuipa kipaumbele sekta ya nishati hasa Gesi Asilia katika
matumizi mbalimbali.
Vilevile amesema ni muda
Muafaka kwa wao kufanya ziara ya kujifunza katika nchi ilizopiga hatua, ili na
wao kama wawakilishi wa wananchi waweze kuongeza msukumo kwa wananchi
wanaowaongoza juu ya Matumizi ya Nishati Safi na Salama ya kupikia kwa lengo la
kuiunga mkono Serikali ya Awamu ya Sita katika azma yake ya kuwataka ifikapo
mwaka 2033, asilimia 80 ya watanzania wote wawe wanatumia Nishati safi na
salama kwa kupikia.
0 Maoni