Hifadhi ya Taifa Mkomazi kuunganishwa na utalii wa Zanzibar

 

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Dastan Kitandula amelielekeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kuiunganisha Hifadhi ya Taifa Mkomazi na utalii wa Zanzibar ili kuongeza idadi ya watalii wanaoitembelea hifadhi hiyo.

Akiwa katika ziara ya kikazi katika hifadhi ya Taifa Mkomazi wilayani Same Mkoani Kilimanjaro, Mhe.Kitandula alisema, "Hakuna haja ya kuachia makundi makubwa ya watalii wanaozulu Zanzibar na kuondoka wakati mmeboresha viwanja vya ndege, hivyo ni wajibu wa TANAPA kutumia fursa na mikakati ya kuwashawishi watalii kutoka Zanzibar kuja kuwaona Faru na wale wanyama wakubwa 5 (The big 5)".

Aidha, Mhe.Kitandula pia ameisisitiza hifadhi hiyo yenye sifa ya kuwa na Faru kujitanga ndani na nje ya nchi hasa katika Bara la Asia ambalo raia wake wanasafiri katika makundi makubwa. Alisema, "Tukibahatika kuwashawishi watalii hawa tutaongeza idadi na mapato na kufikia adhma ya serikali kabla 2025."

Naibu Waziri huyo pia, alilipongeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuvitangaza vivutio inayopelekea kuongezeka kwa watalii, hata hiyo aliwataka kuongeza jitihada za kukabiliana na wanyama waharibifu wakiwemo tembo.

Afisa Mhifadhi Mkuu Kitengo cha Utalii - Mkomazi Happiness Kiemi alimshukuru Mhe. Naibu Waziri na kuahidi kuyafanyia kazi maagizo yote aliyoyatoa ikiwemo utatuzi wa migogoro ya wanyamapori waharibifu.

Mhifadhi Kiemi alisema kuwa hifadhi hiyo imeboresha miundombinu ya utalii ikiwemo ujenzi wa lango la kuingilia wageni pamoja na viwanja vya ndege ili kurahisi safari za kuingia hifadhini na kutoka.

Hifadhi ya Taifa Mkomazi ni mojawapo ya hifadhi zilizoko Kaskazini mwa Tanzania ikisifika kwa kuwa na idadi kubwa ya faru weusi na inapatikana katika mikoa ya Kilimanjaro na Tanga.

Na. Mwandishi wetu - Mkomazi

Chapisha Maoni

0 Maoni