Naibu Waziri Ofisi ya Rais,
Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Ridhiwani Kikwete amesema Mamlaka ya
Serikali Mtandao (eGA) ina jukumu nyeti la kusanifu na kutengeneza mifumo ya
TEHAMA ili iweze kutoa huduma kwa umma kwa haraka na ufanisi.
Mhe.Kikwete ametoa kauli
hiyo leo wakati alipotembelea Ofisi za eGA-Kituo cha Iringa ili kukagua
utendaji kazi wa Mamlaka katika kituo hicho ikiwa ni muendelezo wa ziara yake
ya kikazi mkoani humo.
“Dunia inakwenda kasi na
teknolojia ni kila kitu kwa sasa, hivyo ni muhimu kwa eGA kufanya utafiti,
kubuni na kutengeneza mifumo ya TEHAMA Serikalini kwa ajili ya kurahisisha
utoaji wa huduma kwa umma” amesema Mhe. Kikwete.
Mhe. Kikwete ameongeza kuwa
eGA imeweka juhudi kubwa katika kusimamia TEHAMA Serikalini na imetengeneza na
inaendelea kutengeneza mifumo ya TEHAMA ambayo imewarahisishia wananchi kupata
huduma kwa haraka, mahali popote na kwa gharama nafuu na kuchagiza utawala
bora.
Aidha, Mhe. Kikwete
ameridhishwa na utendaji kazi wa Mamlaka ya Serikali Mtandao katika ofisi zake
zilizopo Iringa na amewataka watumishi wa Mamlaka kwa jumla kuendelea kubuni
Mifumo ya TEHAMA inayotatua changamoto zilizopo nchini pamoja na kuwa wazalendo
kwa maslahi ya Taifa.
Vile vile, amewasisitiza eGA
kuhakikisha mifumo inayotengenezwa na iliyopo inakuwa na uwezo wa kuwasiliana
ili kuleta ufanisi katika kuwahudumia wananchi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi
Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao, Eng. Benedict Ndomba amemshukuru Naibu
Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe.
Ridhiwani Kikwete kwa kutenga muda wake kutembelea kituo hicho cha Iringa na
kuahidi kutekeleza maagizo yote aliyotoa.
0 Maoni