Wanaofanya uhalifu kwenye Ziwa Victoria kusakwa

 

Jeshi la Polisi mkoa wa Mwanza limewaonya watu wanaofanya uhalifu kwenye Ziwa Victoria pamoja na wanaojihusisha na uvuvi haramu na kusema hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

Kamanda wa polisi wa mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa ametoa kauli hiyo wakati akitoa elimu ya kuzuia uhalifu kwa wananchi wa Kata za Bugogwa, Sangabuye, Shibula na Kayenze Wilayani Ilemela ikiwa ni muendelezo wa ziara yake iliyolenga kutoa elimu ya kuzuia uhalifu kwa wananchi wa mkoa huo.

Kupitia kikao hicho Kamanda Mutafungwa akatangaza msako kwa wahalifu wanaopora vyavu za wavuvi na mazao ya uvuvi huku akiahidi kuwachukulia hatua za kisheria watakaobainika.

"Kuanzia leo msako mkali wa kuwasaka wahalifu katika maeneo yote unaendelea, watafute pa kwenda maana inakuja oparesheni kali ambayo itawapa wakati mgumu sana wahalifu tunachoomba kutoka kwenu wananchi ni ushirikiano maana mpaka sasa tuna majina ya wahalifu na tutawafuata popote walipo iwe majini au nchi kavu," amesema Kamanda Mutafungwa.

Katika hatua nyingine Kamanda Mutafungwa amekemea vitendo vya imani za kishirikina ikiwemo Kamchape na Lambalamba na kuwataka wanaoendesha shughuli hizo kujisalimisha wenyewe kwa Jeshi la Polisi kabla hawajaanza kusakwa.

Chapisha Maoni

0 Maoni