Viongozi na Wataalam wa Mkoa wa Dar es Salaam wameanza kupatiwa
mafunzo ya siku mbili ya kujiweka sawa kukabiliana na athari zinazoweza kutokea
endapo mvua kubwa za El-Nino zitanyesha siku za hivi karibuni kwa mujibu wa
utabiri uliotolewa na Mamlaka ya Hali ya hewa hapa nchini.
Akifungua mafunzo hayo jana katika Ukumbi wa NSSF Ilala Boma
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera Uratibu na Bunge Mhe. Jenista Muhagama
amewataka washiriki wote katika kikao kazi hicho kujadiliana kwa kina namna ya
kujipanga na kujiandaa kukabiliana na El-Nino endapo itatokea, ni lazima
kujiratibu na kuwa na vifaa na rasilimali zingine zinazoweza kutumika wakati wa
kulikabili janga hilo.
Mhe Waziri ameutaka Mkoa huo kutumia vyombo vya habari Kutoa
elimu kwa Umma dhidi ya tukio hilo, kusafisha mito na kuimarisha Kingo, kuainisha
maeneo ambayo mara nyingi yana athari Kipindi cha mvua nyingi, kusimamia
matumizi sahihi ya mitaro na mifereji ya maji taka pia kujipanga kuzuia athari
na kutengeneza mipango ya kuzuia madhara pamoja na kushirikisha jamii katika
ulinzi wa mito siharibiwe.
Kwa uande wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe Albert
Chalamila amesema Mhe Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan hataki kuona wananchi
wanapata athari za El-Nino ndio maana ametoa maelekezo mahususi ya kujiandaa,
kujipanga au kuweka mikakati ya kuzuia athari zinazoweka kutokea endapo mvua
hizo zitanyesha.
“Mkoa wa Dar es Salaam tayari umeshaanza kufanya maandalizi
ya kukabiliana na El-Nino ambapo tayari umeshaainisha maeneo hatarishi na
kuanza kusafisha mito kwa mfano mto msimbazi vilevile kazi inaelea kusafisha
mitaro na mifereji pia kuendelea kutoa elimu kwa Umma," alisema RC
Chalamila.
Mwisho Mhe Waziri Jenista Mhagama baada ya kufungua mafunzo
hayo yaliyohudhuriwa na Kamati ya usalama ya Mkoa, Waheshimiwa Wabunge, Wakuu
wa Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri, Makatibu Tawala wa Wilaya, waratibu wa
Maafa kutoka Wilaya zote, Sekretarieti ya Mkoa, wataalam kutoka TARURA, TANROAD
na wadau wengine, amefanya ziara kujionea uhalisia katika maeneo ambayo
yanaweza kuwa na athari kubwa ikiwemo Jangwani, mto Msimbazi, mto Ng'ombe, na
mto mpigi unaotenganisha Mkoa wa Pwani na Dar es Salaam.
0 Maoni