Jeshi la Polisi limetembelea Hifadhi ya Taifa ya Arusha
lengo likiwa ni kujionea vivutio vinavyopatikana katika hifadhi hiyo ambayo
inapatikana ndani ya mkoa wa Arusha sambamba na kuhamasisha watu kutembelea
vivutio hivyo.
Akiongoza zoezi hilo kwa niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi,
Kamishna wa Operesheni na Mafunzo wa Jeshi hilo, CP Awadh Haji alisema wameona
fahari kutembelea hifadhi hiyo yenye vivutio mbalimbali ikiwa ni kuunga juhudi
za Mheshimiwa Rais za kuutangaza utalii wa Nchi yetu.
CP Awadh alibainisha kuwa ziara hiyo itachangia kwa kiasi
kikubwa katika kuimarisha uhusiano, kutatua changamoto za kiusalama baina ya
Jeshi hilo na wadau wengine wanaohusika moja kwa moja kuhudumia watalii.
Sambamba na hilo pia alisema Jeshi hilo limeingia mkataba wa
mashirikiano na Chuo cha Taifa cha Utalii ili kuwajengea uwezo wa kiutendaji
Maafisa, Wakaguzi na Askari ili kuhakikisha wanakwenda kutoa huduma bora kwa
watalii na wageni wote wanaofika nchini.
‘’Dhamira ya Mheshimiwa Rais na Amiri Jeshi Mkuu ni kukuza
Utalii wa nchi yetu na kuongezeka idadi ya watalii nchini, hivyo sisi Jeshi la
Polisi tutahakikisha tunaenda kutoa huduma bora kwa watalii na wageni wanaofika
nchini sambamba na kuimarisha usalama wao,” alisisitiza CP Awadh.
Kwa upande wake Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi hiyo ACC Yustina
Kiwango alisema wamekua na mahusiano mazuri na jeshi la Polisi ambapo mara
nyingi hufanya operesheni za pamoja hali ambayo inapelekea Watalii
wanaotembelea hifadhi hiyo kufurahia mandhari bila ya uwepo wa changamoto za
kiusalama.
Aidha, ametoa wito kwa taasisi nyingine za serikali na za
binafsi kutembelea hifadhi hiyo ili kujionea vivutio vilivyopo sambamba na
kuutangaza utalii wa Nchi yetu.
Ziara hiyo imekuja mara baada ya Jeshi hilo kuingia mkataba
wa mashirikiano na Chuo cha Taifa cha Utalii jana Jijini Arusha ambapo maafisa
wa Jeshi hilo watajengewa uwezo wa kiutendaji wa namna bora ya kuwahudumia
watalii.
Na. Mwandishi wa Jeshi la Polisi
0 Maoni