Vumilia Kasomelo mkazi wa Buchosa wilayani Sengerema mkoani
Mwanza amehukumiwa kwenda jela gerezani miaka mitatu kwa kosa la kumjeruhi kwa
kummwagia maji ya moto mke mwenzake aitwaye Mariam, kisa wivu wa mapenzi.
Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu Mkazi Mwandamizi Evod Kisoki
wa Mahakama ya wilaya ya Sengerema baada ya mshtakiwa huyo kukiri kutenda kosa
hilo
Awali akisoma shtaka hilo kwenye kesi namba 109 ya mwaka huu
mwendesha mashtaka wa serikali Morice Mtoi amesema tukio hilo lilitokea tarehe
26 ya mwezi uliopita majira ya saa tatu usiku katika kijiji cha Lugata tarafa
ya Buchosa wilayani Sengerema ambapo mshtakiwa huyo alimmwagia maji ya moto mke
mwenzake alipokuwa amelala na kumsababishia majeraha.
Mwendesha mashtaka huyo wa serikali amesema Vumilia ametenda
kosa hilo kinyume na kifungu namba 225 cha sheria ya kanuni ya adhabu sura ya
16 toleo la mwaka 2022.
Mshtakiwa huyo baada ya kukiri kutenda kosa hilo Mahakama
ikamhukumu kifungo cha miaka mitatu jela ili iwe fundisho kwa wengine
watakaojaribu kufanya kosa kama hilo.
0 Maoni