TAARIFA KWA UMMA:-
Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya mauaji ya kinyama ya
Mzee Minza Madaha, aliyekuwa mkaazi wa Mtaa wa Ng'wanakiboro, Kata ya
Bunamhala, Tarafa ya Ntuzu Wilaya ya Bariadi mkoa wa Simiyu mnamo tarehe 31
Julai, 2023.
Mama huyo wa miaka 85 aliyekutwa amefariki nyumbani kwake
imeripotiwa amegundulika alikatwa na kitu chenye ncha kali maeneo ya usoni na
sababu inayotajwa ni ushirikina. Tukio hilo linafanyika wakati Serikali pamoja
na Wadau wanaendelea na jitihada za kutokomeza ukatili dhidi ya wazee na
kulinda usalama wao.
Kutokana na juhudi hizo, matukio ya mauaji dhidi ya Wazee
yalikuwa yametoweka ambapo Takwimu zinaonesha mwaka 2021 hakukuwa na tukio
lolote la mauaji. Aidha, kwa miaka ya nyuma matukio hayo yanaonesha kupungua
mathalani; matukio 203 (2017), 93(2018), 74(2019), 54(2020) na 0(2021). Hata
hivyo, matukio haya yalionekana kuongezeka tena hadi 130 mwaka 2022 hivyo bado tunahitaji
ushirikiano na jamii ili kutokomeza matukio haya ili yasitokee na yawe historia
nchini.
Tunaendelea kushirikiana na Serikali ya Mkoa wa Simiyu na
Vyombo vya Dola kuhakikisha wahusika wa mauaji hayo wanakamatwa na
kushugulikiwa kwa mujibu wa Sheria.
Natumia nafasi hii kukemea vikali na kutoa onyo kwa wahusika
wa mauaji hayo na wote wanaopanga kufanya uhalifu wa aina hiyo dhidi ya Wazee
kwa kisingizio cha ushirikina. Aidha natoa rai kwa wanajamii kuchukua jukumu la
kuwalinda na kuwatunza Wazee na kuhakikisha wanakuwa salama katika jamii na
kuepukana na vitendo vya ukatili dhidi yao. Vilevile, nawakumbusha wananchi
kushirikiana na Serikali kwa kutoa taarifa za viashiria vyovyote vya ukatili
kabla madhara hayajatokea.
Dorothy Gwajima (Mb)
WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,
WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM.
0 Maoni