Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, Profesa
Mohamed Janabi amesema hospitali hiyo imeanza kutumia mtambo maakum wa kuyeyusha
damu iliyoganda kwa mtu aliyepata ugonjwa wa kiharusi.
Profesa Janabi amesema hayo jana Jijini Dodoma, na kuongeza
kuwa kwa sasa watu wanaopata ugonjwa wa kiharusi nchini wanatibiwa kwenye kifaa
hicho na wanauwezo wa kupona na kutembea kama kawaida.
“Ukipata kiharusi sasa hivi kama upo Dar es Salaam, ukiletwa
Muhimbili tuna uwezo wa kukuingiza kwenye mtambo na kutoa hiyo damu iliyoganda
na ukapata nguvu na ukatembea kama zamani,” alisema Prof. Janabi na kuongeza, “Haya
ni maendeleo makubwa maana tutapunguza ulemavu kwa wagonjwa hao”.
Profesa Janabi ambaye alikuwa akiongea kwenye mkutano wake na
waandishi wa habari, amesema mtambo huo pia unatumika kutibu wagonjwa
watakaokuwa na tatizo la mishipa ya miguu kuziba.
“Kwa kutumia mtambo huo pia tutatibu kina mama walio na uvimbe kwenye mfuko wa uzazi hatutakuwa na haja ya kufanya upasuaji tunaweza kuyeyusha uvimbe kwenye mashine,” alisema Prof. Janabi.
Kwa upande wa wagonjwa wa saratani, Profesa Janabi amesema
badala ya kupiga dawa ya saratani mwili mzima mtambo huo pia unauwezo wa kugundua
tatizo lilipo na kutibu eneo husika lililokuwa na saratani.
“Ukitumia dawa za
saratani mwili mzima kuna madhara pia lazima upate sasa mtambo utarahisisha
madhara ya dawa itakuwa kidogo, sisi umeshaanza kuufanyia kazi huduma zipo zinapatikana
katika hospitali yetu ya taifa,” alisema Prof. Janabi.

0 Maoni