Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake
na Makundi Maalum Dk. John Jingu amepongeza jitihada zinazofanywa na Wanawake
Wajasiriamali kutoka Mabaraza ya Uwezeshaji wanawake kiuchumi kote nchini
kutokana na ubunifu wanao ufanya katika bidhaa wanazozalisha.
Dk. Jingu ameyasema hayo alipotembelea Banda la Wizara ya
Maendeleo ya Jamii na Wadau wake katika maonesho ya wakulima Nanenane
yanayofanyika Kitaifa mkoani Mbeya.
Dk. Jingu amesema,
shabaha ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum na
wadau wake kushiriki maonesho hayo ni kuonesha kile wanachokifanya lakini pia
kubadilishana uzoefu wa masuala mbalimbali yahusuyo Maendeleo na Ustawi wa
Jamii.
"Kwa sasa bidhaa nyingi za wajasiriamali wetu ni nzuri
ambazo zinatuwezesha kushindana hata kimataifa, hivyo tunapokuja kwenye
maonesho ni katika hali ya kubadilishana uzoefu,'' amesema Dk. Jingu.
Aidha, Dk Jingu amesema wizara itaendelea kushirikiana na
wajasiriamali walioinuka na wanaochipukia ili kila mmoja aone fahari ya uwepo
wa Wizara hiyo.
Katika hatua nyingine, Dk. Jingu ameendelea kuwahimiza watu
wa kada zote kupinga ukatili kwani uwepo wa ukatili ni kikwazo katika kufikia
maendeleo endelevu na usawa wa kijinsia.
"Wenzetu hawa SMAUJATA wanafanya kazi kubwa sana ya
mapambano dhidi ya ukatili rai yangu tuwaunge mkono, wenyewe peke yao
hawataweza tukiunganisha nguvu tutaweza kwa pamoja," amefafanua Dk. Jingu.
Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi
Maalum inashiriki kwa mara ya pili maonesho ya Wakulima Nane Nane yanayoendelea
mkoa Mbeya yanayoongozea na kauli mbiu isemayo. "Vijana na Wanawake ni
msingi imara wa mfumo endelevu wa chakula".
Chanzo: WMJJWM- Mbeya
0 Maoni