Mkazi wa Chamagati Wilaya ya Sengerema Mkoani Mwanza, Maneno
Thomas (35) amehukumiwa kutumikia kifungo cha miaka mitano jela baada ya kutiwa
hatiani kwa kosa la ukatili dhidi ya mtoto wake.
Hukumu hiyo imetolewa leo Agosti 18, 2023 na Hakimu Mkazi
Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya ya Sengerema, Evod Kisoka ambaye alisema Mahakama
baada ya kujiridhisha na ushahidi katika shauri hilo bila shaka imemkuta
mshitakiwa na hatia ya ukatili dhidi ya mtoto wake.
Awali, Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Morice Mtoi aliieleza
mahakama hiyo kuwa Julai 30, 2021, mshtakiwa Thomas alitekeleza ukatili huo wa
kummwagia maji ya moto mikononi, Daniel Maneno (8) katika kijiji cha Chamagati
wilayani Sengerema mkoani Mwanza.
Mtoi alisema mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo kinyume na
kifungu namba 169 (A) (1) na (2) cha Sheria ya Kanuni ya adhabu sura ya 16
toleo la mwaka 2022.
Hata hivyo, mshitakiwa alipopewa nafasi ya kujitetea kuhusu
shtaka linalomkabili, mbali na kukiri pia, aliomba Mahakama impunguzie adhabu
kwani mtoto wake alikuwa ni kero hata kwa majirani kutokana na vitendo vyake
vya udokozi.
Hata hivyo Mahakama imetupilia mbali ombi hilo na kumuamuru
kutumikia kifungo hicho ili iwe funzo kwa watu wengine.
0 Maoni