Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema thamani ya mikopo
inayotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) imeongezeka kutoka
shilingi milioni 776 mwaka 2015 hadi shilingi bilioni 317 Juni mwaka 2023.
Mheshimiwa Majaliwa amesema mafanikio makubwa ni azma ya
Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwainua
wakulima wa Tanzania na kuendeleza Sekta ya Kilimo kwa ujumla.
Amesema hayo jana wakati alipozindua Ofisi ya Benki ya
Maendeleo ya Kilimo Tanzania katika Kanda ya Kusini, Mtwara.
“Ukuaji huo umechagizwa na ongezeko la mtaji kutoka shilingi bilioni 61.09 mwaka 2015 hadi
shilingi bilioni 302.01 katika mwaka 2022.
Ninawapongeza sana kwa hatua hiyo
kwani kadri mtaji unavyoongezeka na uwezo wa kuhudumia wakulima kwa njia ya
mikopo unaongezeka”.
Akizungumza baada ya uzinduzi wa Ofisi hizo Mheshimiwa
Majaliwa amewataka wananchi wa mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma kuchangamkia
fursa ya uwepo wa Ofisi hiyo ya Kanda Mtwara kupata uelewa zaidi kuhusu utaratibu wa kupata mikopo.
“Nendeni mkakope ili mpate vifaa vya kisasa na kupata tija kupitia kilimo”.
“Menejimenti ya Benki na watumishi wa Ofisi ya Kanda ya
Kusini wekeni masharti nafuu katika kutoa mikopo ili kuwezesha mikopo kwa
wakulima, wavuvi na wafugaji kwa wakati,” amesema Mheshimiwa Majaliwa.
Katika Hatua nyingine, Mheshimiwa Majaliwa amesema Benki ya
Maendeleo ya Kilimo Tanzania imetenga shilingi bilioni 35 kwa ajili ya mpango
wa kuwakopesha wakulima wa korosho ili kuendeleza zao hili. “Ni matumaini yangu
kwamba fedha hizi na nyingine ambazo mtaendelea kuwekeza huko zitajikita katika
kufanikisha malengo”.
Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Hamad Hassan Chande ni
amesema kuwa uzinduzi wa Ofisi ya TADB Kanda ya Kusini ni ushahidi tosha wa
dhamira ya dhati ya Serikali ya kuhakikisha kuna kuwa na upatikanaji wa mitaji
kupitia taasisi za fedha na ni kielelezo cha utekezaji wa Mpango wa Taifa wa
Maendeleo wa Taifa.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo
Tanzania (TADB) Frank Nyabundege amesema lengo la kufungua Ofisi katika Kanda
ni kuhakikisha wanafikia wakulima wengi zaidi ambapo mpaka sasa TADB imefungua
ofisi sita katika Kanda Ziwa, Nyanda za Juu Kusini, Kanda ya Magharibi, Kanda
ya Kati na Kanda ya Kusini.
Ameongeza kuwa kupitia uzinduzi wa Ofisi hiyo wataweza
kufikia wakulima, wafugaji na wavuvi kwenye mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma.
“Tutatoa huduma za kibenki zinazoweza kupatikana kwa urahisi, kama vile mikopo
ya kilimo, ujenzi wa viwanda na maghala, mikopo ya matrekta na mashine zingine
za kisasa, pamoja na ushauri wa kitaalamu”.
CHANZO: Ofisi ya Waziri Mkuu
0 Maoni