Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mohamed Mchengerwa
amezindua Kamati ya Ushauri ya Ugawaji wa Vitalu vya Uwindaji wa Kitalii
nchini huku akiitaka kurekebisha kasoro
zote zilizojitokeza siku za nyuma huku akitaka ugawaji ufanyike kwa uwazi ili
kuendana na wakati wa sasa hatimaye tasnia hiyo ichangie kwa kiwango stahiki
kwenye uchumi wa taifa.
Akisoma hotuba yake wakati wa uzinduzi leo Julai 11, 2023
jijini Arusha, Waziri Mchengerwa amesema ameiunda kamati hiyo kwa mamlaka
aliyopewa kwa mujibu wa kifungu cha 38 (1) na (2) ya Sheria ya Uhifadhi wa
Wanyamapori sura ya 283 huku akisisitiza kwamba Kamati hiyo inatakiwa kuboresha changamoto
zote ili tasnia ijiendeshe kibiashara na kupunguza urasimu na mikinzano
isiyokuwa na tija kwa Taifa.
“Ni imani yangu kwamba, kwa kuzingatia ushauri utakaotolewa
na Kamati hii tasnia ya Uwindaji wa Kitalii itazidi kuimarika na kuvutia wawekezaji
wa ndani na nje ya Nchi. Pia Kamati itasaidia kuhakikisha vitalu vyote vinapata
wawekezaji ili kuongezea mapato ya Serikali ikiwa ni pamoja na vitalu 43
ambavyo kwa sasa vipo wazi.” Amesisistiza, Mhe. Mchengerwa
Aidha, amesema anatarajia Kamati hiyo itafanya kazi kwa
ufanisi na weledi katika utendaji kwa kuzingatia kuwa imesheheni wataalamu
kutoka katika nyanja mbalimbali.
Amefafanua kuwa uwindaji wa kitalii unachangia katika pato la
Taifa hususani fedha za kigeni na kwamba kwa wastani, Serikali inakusanya
takriban shilingi Bilioni 30 kwa mwaka kutokana na Uwindaji wa huo na
unachangia ajira za rasmi na zisizo rasmi kwa jamii.
Amesema kiasi hicho ni kidogo ukilinganisha na utajiri wa
raslimali za wanyamapori hapa nchini ambapo ameitaka Kamati hiyo kufanya kazi na kujiwekea malengo makubwa zaidi.
Aidha, ameitaka Kamati hiyo kuzitambua changamoto zinazokabili tasnia hiyo ili kuja
na mikakati ambayo itasaidia kuboresha
sekta hiyo.
Amezitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni pamoja na mabadiliko ya Sera na Sheria za Mataifa yanayoleta watalii wengi wa uwindaji,
mabadiliko ya tabia nchi,uvamizi wa mifugo katika vitalu vya uwindaji wa
kitalii hivyo kuathiri ustawi wa tasnia hii, na kampeni za wapingaji wa uwindaji
wa kitalii ambazo kwa kiasi kikubwa zimeingilia maamuzi ya Mkataba wa Kimataifa
unaosimamia Biashara ya Wanyamapori na Mimea iliyopo Hatarini kutoweka (CITES).
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Ushauri wa Ugawaji
Vitalu
Profesa Jafary Kideghesho, amemhakikishia Waziri Mchengerwa kuwa Kamati yake itafanya kazi kwa weledi ili
kufikia maono na Serikali ya kutaka
tasnia hiyo kuchangia
katia uchumi.
Naye Katibu wa Kamati hiyo ambaye pia ni Kamishna wa Mamlaka
ya Wanyamapori nchini (TAWA) Mabula Nyanda amemshukuru Mhe. Mchengerwa kwa kuiunda Kamati hiyo ambapo amesema itasaidia kuboresha tasnia hiyo kwa kuwa imejumuisha wataalaam waliobobea katika tasnia hiyo.
Mara baada ya uzinduzi huo waziri Mchengerwa ametoa nyaraka
na miongozo mbalimbali kwa wajumbe wote ikiwa ni namna ya kuwakabidhi nyenzo kwa ajili ya
utekelezaji wa kazi zao.
Na John Mapepele
0 Maoni