WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amekuwa miongoni mwa Wakuu wa
Nchi na Serikali waliohudhuria Maonesho ya Gwaride Maalum la Jeshi la Wanamaji
la Urusi yaliyofanyika jana Senatskaya Marina, St. Petersburg, Urusi.
Viongozi hao ni wale walioshiriki Mkutano wa Pili wa Kilele
baina ya Wakuu wa Nchi na Serikali kutoka mataifa ya Afrika na Urusi Jijini St.
Petersburg, Urusi ambako yeye alimwakilisha Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Maonesho hayo yamefanyika ikiwa ni siku ya Jeshi la Wanamaji
la Urusi na maadhimisho ya kukumbuka kuanzishwa kwa jeshi hilo ambayo hufanyika
Julai 30, kila mwaka.
Katika maonesho hayo Rais wa Urusi, Vladmir Putin alipita
kwenye boti maalum akiwasalimia wananchi waliojipanga kwenye kingo za mto
Bolshaya Neva na kupokea salamu za kijeshi. Alipomaliza akavushwa na boti ndogo
kwenda kwenye jukwaa maluum na kuhutubia Taifa.
Baada ya hapo meli na boti za kivita zilipita mbele ya
jukwaa kuu na kutoa heshima. Kisha akaenda kuwasalimia mmoja baada ya mwingine
viongozi wa Afrika waliohudhuria maonesho hayo na baadaye alipanda nao kwenye
boti hiyo maalum.
Chanzo: Ofisi ya Waziri Mkuu
0 Maoni