Watu kadhaa wahofiwa kufa maji kisiwa cha Jugu, ziwa Victoria

 

Watu kadhaa wamezama majini jana maeneo ya kisiwa cha Jugu baada ya mitumbwi miwili midogo waliyokuwa wakisafiria kuzidiwa uzito na kuzama katika ziwa Victoria, ambapo inaarifiwa kuwa bado uopoaji haujaanza kwa kukosekana wataalamu, wazamiaji na vyombo vya uopoaji.

Taarifa zilizonifikia kutoka kijiji cha Buromba, Mwibara-Bunda, mkoani Mara, zinasema katika tukio hilo, zaidi ya watu 15, wengi wao wakidaiwa kuwa ni watoto, bado wapo ndani ya maji tangu jana saa 10:00 jioni walipozama, hali inayohofiwa kwamba tayari watakuwa wamekufa.

Tayari watu 12 waliokolewa, wamelazwa katika Hospitali ya Misheni, Kibara japo hali zao zinaelezwa kuwa si nzuri.

Imeelezwa kwamba, watu hao, washiriki wa Kanisa la Last Church, waliokuwa wakitoka kusali kijiji jirani cha Mchigondo, mtumbwi wa nyuma ulinyunyuka (Ulitoboka) na kuzama, mtumbwi wa mbele ulirudi kuwaokoa, ulipofika eneo la tukio, watu wote waliung'ang'ania kutaka kupanda, nao wakauzamisha.

Eneo hilo la tukio inaelezwa kuna mkondo mkubwa wa maji, wenye mwelekeo wa Majita, hivyo huenda miili ya watu hao wanaohofiwa kufa ikasombwa na mkondo huo wa maji kupelekwa mbali zaidi.

Taarifa zinadai kwamba, asubuhi hii, wananchi watajikusanya kuangalia namna ya kufanya, kwa vifaa hafifu kujaribu kuiopoa miili ya watu hao.

Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mara, Agostino Magere amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuahidi kutoa taarifa zaidi baadaye.

Na. Masau Kuliga Bwire

Chapisha Maoni

0 Maoni