Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa amesema kazi ya uandishi wa habari nchini inasimamiwa na sheria ya huduma za vyombo vya habari na kwamba hakuna mtu anayeruhusiwa kutumia vyombo vya habari kwa maslahi yake binafsi.
Msigwa ameyasema hayo katika kongamano la maadhimisho ya miaka 30 ya Uhuru wa Vyombo vya Habari Duniani mjini Unguja, ambapo amesisitiza kuwa kuna baadhi ya watu wamekuwa wakifanya mzaha na tasnia hoyo jambo ambalo halitavumiliwa.
“ Tasnia ya uandishi wa habari haifungi milango kwamba mtu mwingine haruhusiwi kwenda, muhimu ni kuzingatia maadili ya uandishi, miiko ya uandishi wa habari misingi ya uandishi wa habari, tunachotoa wito kwao waende kwenye vyuo vipo watasoma watapandikizwa taaluma,” amesema Msigwa.
Kwa upande wake Msemaji mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Charles Hillary amesema miaka 30 ni mingi na mambo mengi yamefanyika na vyombo vingi vya habari vimechipuka na kwamba mwananchi anapata habari kwa upeo mkubwa zaidi na hayo ni maendeleo makubwa ya kuigwa mfano.
“Miaka 30 imenikuta mimi nipo kwenye tasnia ya habari kwasababu sasa hivi nina miaka 43 na bado nipo kwenye tasnia ya habari na bado najifunza kila siku” amesema
Akizungumzia kuhusu baadhi waandishi wa habari kufanya kazi kwa kutofuata maadili na tofauti iliyopo kwa sasa kuwa ni kuongezeka kwa waandishi wa habari ambao wengi wao hawajapitia mafunzo ya uandishi wa habari “Mtu akijiona anasauti nzuri au anaweza akapiga picha na kuandika anajiita mwandishi lakini uandishi hauko hivyo inabidi wasome na waelekezwe pia” amesema
Akitolea mfano wake amesema imetokana na kufuata maelekezo ya wasimamizi wake katika tasnia na kuwa shida iliyopo kwa sasa ni vijana kujiona tayari wameshafika na wanaelewa na kupuuza ushauri wa kitaaluma unaotolewa.
0 Maoni