Matumizi ya Sayansi ya tabia yaimarisha maamuzi kuhusu afya ya uzazi

 

Na. Faustine Gimu,Sehemu ya Elimu ya Afya kwa Umma

Matumizi ya Sayansi ya Mabadiliko ya Tabia imeelezwa kuwa ni nyenzo muhimu katika kuimarisha matumizi ya huduma za uzazi wa mpango, kwa kuwa husaidia kubaini sababu zinazochangia maamuzi ya watu kuhusu afya na kuwezesha kubuni afua zinazojibu mahitaji halisi ya jamii.

Akizungumza wakati wa Mafunzo ya Sayansi ya Mabadiliko ya Tabia kwa Waratibu wa Elimu na Hamasa ya Afya kwa Umma, Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto wa Halmashauri, Mkoa na Vituo vya kutolea Huduma za Afya mkoani Kigoma, Mganga Mkuu wa Mkoa , Dkt. Damas Kayera, amesema mafanikio katika kuongeza matumizi ya huduma za uzazi wa mpango yanategemea matumizi ya ushahidi wa kisayansi unaoeleza kwa nini watu hufanya au hushindwa kufanya maamuzi yanayohusu afya zao.

"Sayansi ya Mabadiliko ya Tabia inatuwezesha kuelewa sababu za tabia za watu na kubuni afua zinazozingatia ushahidi. Hii ndiyo njia sahihi ya kuongeza matumizi ya huduma za uzazi wa mpango na kuboresha afya ya uzazi, mama na mtoto," amesema Dkt. Kayera.

Amewataka Waratibu wa elimu na hamasa ya afya kutumia maarifa waliyopata katika mafunzo hayo kubuni na kutekeleza afua zinazozingatia mazingira halisi ya jamii, ili kuongeza uelewa, kuondoa dhana potofu na kuimarisha matumizi ya huduma za uzazi wa mpango.

Mratibu wa Mafunzo hayo, Bw. Simon Nzilibili kutoka Wizara ya Afya amesema mafunzo hayo yana mchango mkubwa katika kuhakikisha huduma za uzazi wa Mpango zinakuwa bora zaidi kwa kuongeza hamasa.

Kwa upande wake, Mwakilishi kutoka Shirika la Afya Duniani(WHO) Tanzania Kitengo cha Elimu ya Afya wakati wa Magonjwa ya Mlipuko na Dharura Bw.Jerry Bikyeombe amesema Mafunzo hayo ni muhimu katika kuhakikisha jamii inakuwa na elimu sahihi na kufanya maamuzi sahihi ya kupata huduma za afya hususan Uzazi wa Mpango.

Kwa upande wao baadhi ya Wanufaika wa Mafunzo hayo akiwemo Mratibu wa Huduma za Afya ya Uzazi, Mama na Mtoto Mkoa wa Kigoma  Bernadeta Peter pamoja na Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza Erick Ernest wamesema mafunzo hayo yatakuwa na chachu kubwa katika elimu ya Afya ya Uzazi wa Mpango Mkoa wa Kigoma.



Chapisha Maoni

0 Maoni