Wahariri Watakiwa Kutumia Kalamu na Sauti Zao Kuimarisha Maadili Nchini

 

KAMISHNA wa Maadili wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Jaji Sivangilwa Mwangesi, amevitaka vyombo vya habari nchini kuendelea kushirikiana na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma katika kukuza uadilifu na uwajibikaji miongoni mwa viongozi wa umma, akisisitiza kuwa jukumu hilo linahitaji ushiriki wa wadau mbalimbali wakiwemo wahariri na wanahabari.

Katika hotuba yake iliyosomwa na Kaimu Kamisha wa Maadili Kassim Mkwawa katika Kikao na Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Jaji Mwangesi alisema ushirikiano kati ya Sekretarieti ya Maadili na vyombo vya habari umeendelea kuzaa matunda kwa miaka minne iliyopita, kupitia utoaji wa elimu kuhusu Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya mwaka 1995 na kubadilishana mawazo yanayosaidia kuimarisha uadilifu nchini.

Alisema katika mwaka wa fedha 2025/26 unaokaribia kumalizika, Sekretarieti hiyo imefanya ziara katika kanda zake nane kwa lengo la kukutana na wahariri wa maeneo mbalimbali na kujadili namna bora ya kuendeleza ushirikiano katika kukuza maadili ya viongozi wa umma, huku akiwapongeza wahariri kwa mchango wao katika kuibua mijadala chanya inayolenga kuimarisha uwajibikaji.

Jaji Mwangesi alisema Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma ilianzishwa kwa mujibu wa Ibara ya 132 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma Na. 13 ya mwaka 1995, huku akieleza kuwa taasisi hiyo ina jukumu la kutoa elimu ya maadili kwa umma kupitia vyombo vya habari, semina, makongamano, maonesho na mikutano mbalimbali.

Aidha, aliwataka wahariri na wanahabari kutumia taaluma yao katika kuibua na kuripoti masuala yanayohusu ukiukwaji wa maadili ya viongozi wa umma, akibainisha kuwa zipo njia mbalimbali zinazoweza kutumika kuwasilisha taarifa hizo ikiwemo barua pepe, mfumo wa mrejesho wa kielektroniki na simu, huku akisisitiza kuwa kazi ya kujenga uadilifu ni jukumu la kila Mtanzania.

Alisema kuwa uwepo wa viongozi waadilifu una manufaa makubwa kwa Taifa na vizazi vijavyo kwa kuhakikisha rasilimali za nchi zinawanufaisha wananchi wote, na kuwataka wahariri kuendelea kutumia kalamu na sauti zao kujenga umoja, mshikamano na kudumisha amani nchini, huku akivipongeza vyombo vya habari kwa kuendelea kuzingatia weledi na maadili ya taaluma katika kulinda maadili ya Mtanzania licha ya changamoto za utandawazi.

Kwa upande wa Wahariri wametaka maboresho kwenye sheria iweze kuruhusu mali za viongozi wa serikali kuwekwa hadharani kwenye mitandao ya kijamii ili kila mmoja ajue anachokimiliki kiongozi wake.

Akizungumza katika kikoa hicho jijini Da es Salaam Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) Deodatus Balile, amesema ifike hatua mali za viongozi ziweke hadharani akisema hatua hiyo itasaidia kuondoa minongono ya wananchi dhidi ya viongozi.

Katibu wa Idara ya Ukuzaji Maadili ya Viongozi wa Umma, Waziri Kipacha, amesema sheria ya maadili ya viongozi wa umma na kanuni zake, hasa ya tamko la rasilimali, maslahi na madeni imeweka utaratibu wa wananchi kukagua taarifa za mali za viongozi.

Katibu Usimamizi wa Maadili kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Kassim Mkwawa, amesema malalamiko ni mengi lakini hatua wanayoichukua ni kuyafanyia kazi.

Lakini tunapofanya uchunguzi hua hatusemi, uchunguzi ni siri, hadi hapo itakapolazimika kusema, japo kuna haja kubwa ya kuelimisha jamii kuhusu taratibu za kisheria,” amesema.


Chapisha Maoni

0 Maoni