TANAPA yapokea tuzo ya Gis kutoka Esri Eastern Africa

 

Na. Brigitha Kimario- Arusha

Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limepokea tuzo ya Mifumo ya Taarifa za Kijiografia (GIS) kwa Ukanda wa Africa kutoka Esri Eastern Africa, baada ya kutambuliwa kwa umahiri wake katika matumizi ya teknolojia ya ArcGIS katika shughuli za uhifadhi na utalii.

Akikabidhi tuzo hiyo leo Juni 18, 2026 Mwakilishi wa Esri Eastern Africa na Meneja wa Mafanikio kwa Wateja (Customer Success Manager), Bi. Monica Mwanzia, alisema TANAPA imeibuka mshindi kutokana na matumizi bora ya teknolojia ya GIS katika ukusanyaji wa taarifa za uwandani (spatial data collection), kuchakata (spatial analysis) na uandaaji wa ramani (map production).

Akizungumza kwa niaba ya Kamishna wa Uhifadhi TANAPA, Naibu Kamishna wa Uhifadhi na Maendeleo ya Biashara Massana Mwishawa alisema kuwa ushindi wa tuzo hiyo ni uthibitisho wa mafanikio makubwa ambayo TANAPA imeyapata katika matumizi ya teknolojia za kisasa.

Kamishna Mwishawa alisema, “Ushindi huo wa tuzo ya GIS kwa Ukanda wa Afrika ni heshima kwa Taifa na TANAPA kwa ujumla ambao unatupa motisha na ari ya kuendelea kuwekeza katika matumizi sahihi ya mifumo ya GIS ili kuendana na kasi ya Maendeleo ya Sayansi na Tecknolojia Duniani.”

Aidha, alibainisha kuwa TANAPA imeendelea kutumia teknolojia ya GIS kwa zaidi ya miaka 15 tangu mwaka 2011, ambapo imekuwa ni nyenzo muhimu katika kutatua migogoro ya matumizi ya ardhi kati ya hifadhi na maeneo jirani, kukusanya na kuchambua data za kijografia, kuongeza ufanisi wa maamuzi ya kiutendaji na kuimarisha usimamizi wa rasilimali za uhifadhi.

Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi na Mkuu wa Kitengo cha GIS TANAPA, Dkt. Abel Mtui, alisema kuwa mfumo huo umeimarisha uwajibikaji na ufanisi kwa watumishi wanaotekeleza majukumu yao uwandani.

Vilevile, Kamishna Mtui aliongeza, “Teknolojia ya GIS inawezesha kufuatilia maeneo yaliyokaguliwa, ukubwa wa maeneo yaliyofanyiwa doria, kubaini mtawanyiko wa wanyamapori na kutambua maeneo yenye changamoto za ujangili. Pia mfumo huo husaidia kutambua maeneo yenye fursa za uwekezaji katika malazi ya watalii, miundombinu ya barabara na viwanja vya ndege.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 1959, TANAPA imeendelea kuimarisha matumizi ya teknolojia mbalimbali za kisasa ikiwemo GIS, TEHAMA na mifumo mingine ya kidijitali inayotumika katika shughuli za uhifadhi, utalii, ukusanyaji wa mapato na manunuzi. Matumizi ya teknolojia hizo yameongeza kasi kwa TANAPA kujizolea tuzo mbalimbali maarufu za kitaifa na kimataifa.



Chapisha Maoni

0 Maoni