Na Mwandishi Wetu
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana
wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Kagera, Faris Buruhani, ametoa
mwito mzito kwa vijana nchini kote kusimama imara kama walinzi wa
amani na utulivu, huku akiwaonya vikali kujiepusha na makundi yenye
nia ovu yanayoshawishi jamii kuvunja sheria na kuhatarisha usalama wa
taifa.
Akizungumza kwa nyakati tofauti katika kata mbalimbali
mkoani hapa wakati wa mwendelezo wa Operesheni ya Vijana Daka Fursa
na Samia yaani VIDAFUSA Awamu ya Pili, Buruhani alisema kuwa amani na
mshikamano ndio nguzo pekee zinazowezesha nchi kupiga hatua za
kimaendeleo, hivyo vijana hawapaswi kukubali kufuata mkumbo unaolenga
kuichoma moto nchi na kubomoa yaliyojengwa.
Kiongozi huyo wa
vijana alifafanua kuwa ustawi wa kiuchumi na kijamii unaoshuhudiwa
hivi sasa katika sekta mbalimbali nchini unahitaji ulinzi wa hali ya
juu kutoka kwa nguvu kazi ya taifa, na kuwataka vijana kutambua kuwa
wana nafasi ya msingi sana katika kujenga au kubomoa mustakabali wa
Tanzania.
Buruhani alisisitiza kuwa badala ya vijana kupoteza
muda na nguvu zao kwenye majukwaa yanayochochea chuki, fujo na
mifarakano, wanapaswa kukimbilia na kuzichangamkia fursa mbalimbali
zinazotolewa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais
Samia Suluhu Hassan ikiwemo mikopo ya uwezeshaji, elimu ya
ujasiriamali na programu maalumu za kukuza vipaji na uchumi
wao.
Aliongeza kuwa operesheni hiyo ya VIDAFUSA itaendelea
vijijini na mijini mkoani Kagera ili kuwajengea vijana uwezo wa
kujikwamua kiuchumi na kuwapa elimu ya uzalendo ili wasiweze
kushawishiwa kirahisi na watu wanaotaka kuvuruga utulivu wa nchi kwa
maslahi yao binafsi ya kisiasa na kijamii.

0 Maoni