Mchambuzi wa masuala ya uongozi, uchumi na siasa nchini, Dkt. Netho Ndilito amesema ripoti ya Tume ya kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 imeleta mwanga mpya kuhusu hali halisi ya taifa na changamoto zilizokuwa zikijadiliwa kwa muda mrefu.

Amesema baada ya kupitia maoni ya Watanzania, wanamitandao na wachambuzi mbalimbali, ameona ripoti hiyo ni nyaraka muhimu iliyofichua mambo makubwa yenye maslahi kwa taifa.

Kwa mujibu wake, ripoti hiyo imeliponya taifa kwa kuweka wazi ukweli ambao kwa muda mrefu haukupata nafasi ya kujadiliwa hadharani, ikiwemo kufichua nia na dhamira za baadhi ya watu waliotamani vurugu kabla, wakati na baada ya uchaguzi.

Aidha, ameeleza kuwa ripoti hiyo imeweka bayana upotoshaji na taarifa zisizo sahihi zilizokuwa zikisambazwa na baadhi ya watu wasiolitakia mema taifa, huku wakitamani kuona nchi ikiingia kwenye machafuko.

Pia amesema ripoti hiyo imeonesha namna Watanzania wengi wanavyoipenda nchi yao, kuiamini serikali yao na kutokuwa tayari kushawishika kuivuruga amani, umoja na mshikamano wa taifa.

Vilevile, imebainisha uimara wa serikali pamoja na ukomavu wa vyombo vya ulinzi na usalama katika kushughulikia masuala ya ndani kwa weledi na utulivu.

Dkt. Ndilito amewapongeza Watanzania kwa kuendelea kudumisha umoja, upendo, mshikamano na amani, akisisitiza kuwa huo ndiyo msingi wa heshima ya taifa kwa muda mrefu.