CHAMA cha Wananchi CUF kimetoa msimamo wake kuhusu ripoti ya Jaji Othman Chande iliyohusu matukio ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 29, kikitaka serikali kujikita zaidi katika maridhiano ya kweli na mchakato wa uponyaji wa taifa.
Chama
hicho kimesisitiza umuhimu wa kuwasaidia waathirika wa vurugu,
ikiwemo kuwapatia matibabu ya kimwili na kisaikolojia pamoja na
msaada wa kijamii.
Akizungumza kwa mara ya kwanza na waandishi
wa habari tangu achaguliwe kuwa mwenyekiti wa chama hicho, Mwenyekiti
wa CUF Taifa, Mirambo Kamili Yusufu, alisema chama hicho hakioni
ulazima wa kujadili kwa kina ripoti hiyo kwa kuwa ni ripoti ya Rais
iliyotengenezwa kitaalamu kwa lengo la kudumisha amani ya nchi.
Hata
hivyo, alisisitiza kuwa maridhiano ya kweli na uponyaji wa taifa ni
mambo ya msingi, sambamba na hitaji la kuwepo kwa Tume Huru ya
Uchaguzi na Katiba mpya.
Aidha, Yusufu alizungumzia hali ya
kisiasa na kiusalama Mashariki ya Kati, akieleza kuwa migogoro
inayoendelea, ikiwemo vita vinavyohusisha Iran, Marekani na Israel,
ina athari za kiuchumi duniani.
Alisema kuwa endapo chama hicho kingekuwa madarakani, kingeimarisha mfuko wa dharura ili kupunguza athari hizo kwa wananchi, hususan kupanda kwa gharama za maisha kama nauli na bei za bidhaa.

0 Maoni