Mkurugenzi
Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K.
Bakari, tarehe 19 Mei 2026 alifanya vikao vya mashauriano na wadau wa
sekta ya anga katika Makao Makuu ya TCAA yaliyopo Banana, Ukonga
jijini Dar es Salaam.
Vikao hivyo vilifanyika katika vipindi
viwili tofauti ambapo kikao cha asubuhi kilihusisha wamiliki na
waendeshaji wa mashirika ya Ndege ya ndani, huku kikao cha mchana
kikihusisha wamiliki na waendeshaji wa mashirika ya Ndege kutoka nje
yanayokuja na kufanya shughuli zao nchini Tanzania.
Vikao
hivyo vilitoa fursa kwa wadau kufanya majadiliano ya wazi na ya
kujenga na uongozi wa TCAA, ambapo walitoa maoni, uzoefu na kueleza
changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya anga.
Akizungumza
wakati wa ufunguzi wa vikao hivyo, Dkt. Bakari alijitambulisha rasmi
kwa wadau na kusisitiza dhamira yake pamoja na menejimenti ya TCAA
kuhakikisha sekta ya anga nchini inaendelea kufanya kazi kwa ufanisi
na kukua zaidi.
Alieleza kuwa TCAA itaendelea kushirikiana kwa
karibu na wadau wote wa sekta hiyo ili kuboresha utoaji wa huduma na
kuimarisha maendeleo ya sekta ya anga nchini.
Dkt. Bakari pia
aliwaeleza wadau kuwa TCAA ipo katika mchakato wa kuboresha na
kuoanisha mifumo yake ili kurahisisha michakato ya biashara na
kuongeza ufanisi wa huduma. Aliwataka wadau kuwa tayari kuunga mkono
maboresho hayo pindi yatakapohitajika.
Aidha, alitangaza kuwa
TCAA inapanga kuanzisha namba maalum ya bure ya simu pamoja na dawati
maalum la huduma kwa Wateja ili kurahisisha mawasiliano na
kushughulikia changamoto zao kwa haraka zaidi.
Katika
majadiliano hayo, wadau waliwasilisha mapendekezo, maoni pamoja na
changamoto mbalimbali zinazoathiri shughuli za sekta ya anga. Akijibu
hoja hizo, Dkt. Bakari aliwahakikishia wadau kuwa TCAA imepokea na
kuzingatia masuala yote yaliyowasilishwa na kwamba menejimenti ya
mamlaka hiyo itashirikiana kwa karibu na wadau kuhakikisha changamoto
hizo zinapatiwa ufumbuzi stahiki kwa ajili ya maendeleo endelevu ya
sekta ya anga nchini Tanzania.
Akihitimisha vikao hivyo, Dkt.
Bakari alisisitiza kuwa TCAA imejipanga kuhakikisha sekta ya anga
nchini Tanzania inaendelea kukua, akieleza kuwa kama sekta ya anga
inavyofanya kazi saa 24 kwa siku, vivyo hivyo TCAA ipo tayari
kuwahudumia wadau wake wakati wote.
Vikao hivyo vya
ushirikishwaji wa wadau vinaendelea.

0 Maoni