Mawakili wa Serikali wametakiwa
kuendelea kuwa watetezi wa Serikali katika uendeshaji wa mashauri ya
madai na usuluhishi kwa niaba ya Serikali na taasisi zake.
Hayo
yameelezwa na Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt. Ally Possi wakati
akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa watumishi wa Ofisi ya Wakili Mkuu
wa Serikali uliofanyika jijini Arusha.
“Mawakili wa Serikali
wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali mtambue mna jukumu la kuendelea
kuitetea Ofisi na Serikali mahakamani katika uendeshaji wa mashauri
ili tulinde maslahi ya taifa letu,” amesema Dkt. Possi.
Pia,
amewataka watumishi wa Ofisi hiyo kuendelea kudumisha umoja,
mshikamano na upendo ndani ya taasisi kwa kuwa hii ni afya kwa
taasisi na nchi yetu na hili liwe mpaka chini kwa watumishi
wote.
Naibu Wakili Mkuu wa Serikali, Bi. Alice Mtulo
aliwapongeza watumishi wa Ofisi hiyo kwa ushirikiano wa pamoja na
mwenendo huu unaendelea kuijengea heshima Ofisi na ina akisi ukomavu
wa Ofisi.
“Kila kiungo ni muhimu, mchango wa kila mtumishi
ni muhimu ili kuhakikisha kuwa tunafikia malengo yaliyowekwa,”
amesisitiza Bi. Mtulo.
Bi. Mtulo amewaeleza watumishi hao kuwa
Serikali ina matarajio makubwa kutoka kwao. Hivyo, kila mmoja
atekeleze majukumu yake kwa kuzingatia sheria, taratibu na kanuni za
utumishi wa umma, maadili ya utumishi wa umma na viwango vya taaluma
tulivyojiwekea ili tuwe na utamaduni wa kuendelea kufanya kazi kwa
bidii na weledi kwa manufaa ya taifa kwa ujumla.
Mkutano huo
hufanyika mara moja kwa mwaka ili kuwakutanisha watumishi wote kwa
lengo la kujadiliana kuhusu mafanikio yaliyopatikana wakati wa
utekelezaji majukumu, changamoto, kupata mafunzo mbalimbali ya
kuimarisha utendaji kazi na ustawi wa mtumishi mmoja mmoja ili
kujenga Ofisi yenye mshikamano na mazingira mazuri ya kazi.
Mkutano
huo umefanyika kwa siku mbili tarehe 21 na 22 Mei, 2026 na
kuwakutanisha watumishi wote wa Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali
zilizopo kwenye mikoa 18 Tanzania Bara.


0 Maoni