Mafanikio makubwa ya timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars,
katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika 2025 yameendelea kuibua mjadala
mzito miongoni mwa mashabiki wa soka katika ukanda wa Afrika Mashariki na
kwingineko.
Wakati Tanzania ikisherehekea hatua hiyo kubwa wapo baadhi
ya watu na majirani wanaoonekana kuteseka na kusononeka kutokana na mafanikio
hayo ambayo kwa uhakika si ya bahati mbaya bali ni matunda ya uwekezaji mkubwa
uliofanywa katika miundombinu ya michezo na usimamizi wa michezo ikiwamo soka.
Ni vyema wanaobeza wakaelewa kuwa mafanikio ya Taifa Stars
ni matokeo ya amani ya kudumu iliyopo nchini Tanzania ambayo imetoa fursa ya
kuendeleza vipaji vya vijana na kuifanya ligi kuu ya Tanzania kuwa miongoni mwa
ligi bora na zenye mvuto mkubwa barani Afrika jambo linalozalisha wachezaji
makini na wenye ushindani wa hali ya juu.
Kabla ya michuano hii kuanza baadhi ya majirani waliibeza
Taifa Stars wakiamini ingeondolewa mapema katika hatua za awali na hata baada
ya timu hiyo kufuzu hatua ya kumi na sita bora bado kejeli zimeendelea
mitandaoni zikidai kuwa imefuzu bila kushinda mechi yoyote jambo ambalo ni
tafsiri ya wivu wa mafanikio.
Hata hivyo, kufuzu kwa Taifa Stars kumeibua tafakuri mpya
miongoni mwa wachambuzi wa kimataifa ambao wanakiri kuwa Tanzania imepiga hatua
kubwa kutokana na ligi yake ya ndani kuwa imara na kutoa idadi kubwa ya
wachezaji wanaocheza michuano hiyo mikubwa.
Wachambuzi kutoka nchi jirani kama Kenya wameanza kukiri
hadharani kuwa wakati Tanzania ikifuzu AFCON mara kwa mara tangu 2019 hadi 2025
kwa misingi ya ushindani wao wamebaki wakitegemea bahati ya uenyeji au kutoa
visingizio huku wakishindwa kuwekeza kama ilivyofanya Tanzania.
Mafanikio ya soka nchini Tanzania yanajidhihirisha kupitia
maendeleo ya klabu za ndani kimataifa na mifumo ya kukuza vipaji vya vijana
ambayo imeifanya Taifa Stars kuwa timu iliyokomaa yenye mwelekeo sahihi na
mustakabali mzuri.
Kuteseka kwa majirani na baadhi ya watu mitandaoni ni
ishara kuwa Tanzania imekuwa mfano wa kuigwa na somo kubwa kwa ukanda huu kuwa
hakuna mkato katika soka la kisasa bali uwekezaji wa muda mrefu, mipango
thabiti na usimamizi bora ndiyo njia pekee ya kupata mafanikio endelevu.
Badala ya kutoa kauli za kubeza na kukejeli ni vyema wadau
wa soka wakajifunza kutoka Tanzania jinsi ya kutumia amani na rasilimali
zilizopo kuinua kiwango cha mchezo huo na kuacha tabia ya kupuuza hatua kubwa
zinazopigwa na taifa hili.
Ujumbe kwa wale wanaoposti maoni ya dhihaka na lugha
zisizofaa mitandaoni ni kwamba chuki haitawasaidia kupata mafanikio bali
kuelewa kuwa michezo ni sayansi na Tanzania imeshafanya ugunduzi wa dawa ya
ushindi kupitia umoja na uwekezaji.
Jamii inapaswa kupuuza jumbe hizo za kejeli za uchochezi na
badala yake iendelee kuishangilia Taifa Stars ambayo kwa sasa ni kielelezo cha
ukomavu wa soka la Afrika Mashariki huku ikiendelea kuchanua katika hatua za
mtoano. Hakika kila tone la jasho la wachezaji wa kitanzania uwanjani ni
kielelezo cha amani tuliyonayo na dhamira ya dhati ya serikali na wadau wa soka
kuhakikisha bendera ya Tanzania inapepea juu kileleni mwa mafanikio ya soka
barani Afrika na duniani kwa ujumla.

0 Maoni