Tanzania Bloggers
Network (TBN) imetoa salamu maalumu kwa Watanzania katika kuadhimisha miaka 64
ya Uhuru leo, Desemba 9, ambapo imesisitiza umuhimu wa kutafakari safari ya
maendeleo ya Taifa na nafasi ya kila Mtanzania katika kuendelea kulijenga.
Akitoa salamu
hizo, Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, amesema kuwa siku ya Uhuru si tukio la
mapumziko pekee, bali ni siku ya kukumbuka misingi iliyowekwa na waasisi wa
Taifa katika kutafuta, kudumisha na kulinda Uhuru wa Tanzania.
Msimbe
aliwakumbusha Watanzania kauli ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius
Kambarage Nyerere, aliyewahi kusisitiza kuwa Uhuru hauwezi kukamilika pasipo
kujitegemea.
“Uhuru hauwezi
kukamilika pasipo kujitegemea. Hatuwezi kuitwa huru kama tunategemea wengine
kutupatia mahitaji yetu ya kimsingi,” alimnukuu Mwalimu Nyerere.
Amani na Utulivu:
Nguzo za Maendeleo
TBN imeeleza kuwa
mafanikio ambayo Tanzania imeyapata katika miaka 64 ya Uhuru yametokana na
misingi ya amani, utulivu na mshikamano miongoni mwa wananchi.
Msimbe alisema
kuwa bila misingi hiyo, jitihada za Taifa katika kushughulikia changamoto za
ujinga, umaskini na maradhi haziwezi kufanikiwa.
Akinukuu maneno ya
Rais mstaafu Benjamin William Mkapa, Msimbe alisema:
“Amani si kitu cha
asili, tunahitaji kuilinda na kuitunza kila siku. Bila amani, hakuna maendeleo
ya kweli.”
TBN imeonya kuwa
vurugu na uchochezi vyaweza kudhoofisha jitihada za kizazi kilichopita na
kizazi cha sasa katika kusukuma mbele gurudumu la maendeleo.
Kila Kizazi na
Zama Zake
Katika salamu
hizo, TBN pia iligusia umuhimu wa kuheshimu zama tofauti za uongozi, ikinukuu
kauli maarufu ya Rais Mstaafu Hayati Ali Hassan Mwinyi:
“Kila utawala na
zama zake. Kila kiongozi na mchango wake katika ujenzi wa Taifa hili.”
Mwenyekiti huyo
alisema kuwa chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, nchi inaendelea
kusimamia dira ya 4R Reconciliation,
Resilience, Reforms, and Rebuilding ambayo inalenga kuimarisha maridhiano, mageuzi
na ustawi wa Taifa.
Wito kwa
Watanzania
TBN imewataka
Watanzania kutumia uhuru wa kujieleza kwa kujenga, si kubomoa, kwa kusisitiza
umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii, kudumisha amani na kuepuka kutumika kama
chombo cha kuchochea migawanyiko.
“Watanzania,
tunayo nafasi ya kuzungumza, tuzungumze. Tusiitumie nafasi hiyo kubomoa Taifa
bali kulijenga,” alisema Msimbe.
TBN imemalizia kwa
kuwatakia Watanzania wote maadhimisho mema ya miaka 64 ya Uhuru, ikimalizia na
kauli mbiu:
Tanzania Kwanza,
Kazi na Utu Tusonge Mbele

0 Maoni